Tuesday, August 4, 2015



YALIANZA maneno, lakini sasa Jose Mourinho na Arsene Wenger wanaelekea kubaya zaidi. Juzi kila kitu kilikuwa wazi kwamba makocha hawa wana bifu zito zaidi ya ilivyokuwa inafikiriwa awali.
Arsene Wenger hatimaye alifanikiwa kukata uteja wa kucheza mechi 14 bila ya kushinda dhidi ya Mourinho, baada ya bao murua la winga wake, Alex Oxlade-Chamberlain kuipa timu yake taji la Ngao ya Jamii.
Hata hivyo, mechi hiyo iliingiwa na doa baada ya Wenger kukwepa kumsalimia Mourinho mara mbili, huku mara ya pili ikiwa wazi zaidi baada ya Mourinho kujipanga kuwasalimia wachezaji wote wa Arsenal na benchi la ufundi, lakini Wenger akapita mgongoni kwake na kuwafuata wachezaji wake.
Mourinho amesikitishwa na kitendo hicho huku akimlaumu Wenger kwa kuukwepa mkono wake mara mbili, ingawa Wenger amepuuza jambo hilo.
“Nilikuwa nafanya vile kwa ajili ya heshima ya klabu yangu na heshima yangu kama meneja na inabidi nifanye vile kwa klabu ambayo ni mshindi, unawasubiri katika namna hauwezi kukosa kumwona mtu yeyote na hakuna atakayekosa kukuona,” alisema Mourinho.
“Kila mchezaji alikuja katika mwelekeo wangu kitu ambacho kilikuwa rahisi kwangu kufanya, sasa kama kuna watu wengine hawakuja katika mwelekeo wangu hilo siyo tatizo langu, siyo habari, siyo mwisho wa dunia na sina tatizo na hilo,” aliongeza Mourinho.
“Nilifanya kazi yangu, kazi ambayo klabu yangu inastahili niifanye kwa hadhi yangu kama bosi pindi ninapopoteza mechi ya Ngao ya Jamii au kombe lolote lile.”
Hata hivyo, Wenger alipuuza madai hayo ya Mourinho huku akidai kwamba alipeana mikono na watu wachache aliojisikia kupeana nao mikono na hiyo siyo habari.
“Nilipeana mikono na watu wachache leo baada ya mechi, lakini hakuna kitu cha maana hapo. Naamini katika kazi ambayo inabidi uwaheshimu watu na umheshimu kila mmoja,” alisema Wenger.
Wenger pia alikanusha madai ya Mourinho kwamba Wenger aliachana na falsafa yake ya kucheza soka la kushambulia na kuamua kucheza soka la kujihami kwa ajili ya kulinda bao la Chamberlain.
“Hakuna tulichoachana nacho. Tulijilinda kwa sababu kulikuwa na kikwazo cha kisaikolojia dhidi ya Chelsea kwa wachezaji wangu. Walitaka kulinda ushindi wetu wa 1-0 kuliko kucheza,” alisema Wenger.
“Inabidi tukubali hilo. Sidhani kama hilo ni kuachana na falsafa yetu, ni kweli kwamba ni mechi ambayo tulitaka kushinda na ndiyo maana tulifanya hivyo. Najivunia hilo,” aliongeza kocha huyo Mfaransa.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe