Tuesday, August 4, 2015



KOCHA mkuu wa Simba, Dylan Kerr, ana changamoto kubwa visiwani hapa, kazi yake si rahisi hata kidogo.
Licha ya timu yake kushinda mechi tatu za awali za kirafiki, bado ana kazi kubwa kuhakikisha anapata timu bora zaidi.
Simba ilicheza mechi za kirafiki dhidi ya Kombaini ya Zanzibar na kushinda 2-1, ikaifunga Braxeria 4-0 na kisha kuifunga Polisi Zanzibar mabao 2-0.
Hata hivyo licha ya matokeo hayo kuna mambo bado yanampasua kichwa kocha Kerr. Kocha huyo raia wa Uingereza pamoja na yule wa viungo, Mserbia Dusan Momcilovic, wana kibarua kizito kuhakikisha kuwa timu hiyo inakuwa bora kuliko wapinzani wao wakubwa Yanga na Azam.
Mwanaspoti ambayo imeweka kambi pamoja na timu hiyo visiwani hapa inakuletea mambo ambayo ni changamoto kubwa kwa kocha huyo pamoja na wasaidizi wake.
Uwiano wa kikosi
Kwa bahati mbaya Simba ina viungo wengi kuliko wachezaji wa idara nyingine. Timu hiyo ina viungo zaidi ya 10. Ina Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto, Said Ndemla, Abdi Banda, Peter Mwalyanzi, Michael Mgimwa, Awadh Juma, Mbarouk Yusuf, Simon Sserunkuma na kiungo anayejaribiwa Justice Mujabvi.
Wingi huu wa viungo unamfanya Kerr kukosa uwiano sahihi wa kikosi chake. Uchaguzi mpana alionao katika safu ya kiungo haupo katika nafasi nyingine. Hapa ana kazi kubwa ya kufanya ili kuhakikisha anapata kikosi chenye uwiano mpana.
Kusuka kombinesheni
Simba sasa ina wachezaji wengi wazuri, lakini bado wameshindwa kucheza kwa uelewano mkubwa. Hii inamaanisha kuwa Kerr ana kazi ngumu ya kusuka kombinesheni mbalimbali katika timu yake.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe