Tuesday, August 4, 2015



HATIMAYE Azam imeweka historia kwa kulibeba kwa mara ya kwanza taji la michuano ya Kombe la Kagame iliyomalizika juzi Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Awali mashabiki walishuhudia ushindani ambao ulilifanya taji la michuano hiyo kuwa gumu kubashiri kwamba nani angeweza kuibuka mshindi hasa kwa timu za Gor Mahia ya Kenya, KCCA ya Uganda, Al-Khartoum ya Sudan na wenyeji Azam.
Hali hiyo ilitokana na namna ushindani ulivyokuwa na wengi walipata tabu kuitabiria Azam ubingwa hata baada ya ushindi wake dhidi ya Yanga katika mechi ya robo fainali.
Kwa baadhi ya mashabiki ushindani ambao ulianza kuonekana katika hatua ya robo fainali ni kati ya mambo ambayo yanapendeza kuonekana katika mashindano ya Kombe la Kagame tangu hatua ya makundi.
Hatua ya makundi isiwe mteremeko kwa baadhi ya timu kujihakikishia ushindi wa mabao mengi kwani jambo hilo linachangia kushusha au kupoteza hadhi ya mashindano haya ambayo yanashirikisha timu za nchi tofauti.
Ni matumaini yetu kwamba katika mashindano yajayo timu zitajipanga kuhakikisha zinatoa ushindani jambo ambalo litayafanya mashindano kuwa na mvuto na kuanzia hatua za mwanzo na hivyo kusaidia kuinua soka la Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Kwa Azam ushindi ambao wameupata ni kati ya mambo ambayo mashabiki wa timu hiyo na mashabiki wa soka nchini kwa jumla wamekuwa wakiyasubiri au kuyatarajia kwa muda mrefu sasa.Azam ni timu ambayo imefanya uwekezaji wa hali ya juu kuanzia kwa wachezaji na mambo mengine ya msingi katika soka hivyo ubingwa wa Kagame ni haki yao na ni kati ya mambo ambayo yanapendeza kusikia wameyafanikisha.
Hata hivyo, pamoja na ukweli huo, pia tungependa kuwakumbusha viongozi na wachezaji wa Azam kwamba bado wana kazi ya kufanya baada ya Kombe la Kagame.
Kwa hadhi na uwekezaji uliofanywa na Azam ni muhimu wakaweka mikakati ya kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye mashindano ya Afrika.
Kombe la Shirikisho au Ligi ya Mabingwa Afrika ni aina ya mashindano ya kiwango cha Azam kushiriki na kuhakikisha wanafanya vizuri na si kubweteka na Kombe la Kagame. Ni kweli kwamba Kombe la Kagame ni faraja mojawapo kwa timu hiyo na mashabiki wake lakini ni vyema timu hiyo ikaanza kusaka heshima yake Afrika, hiyo ndiyo hadhi yao na si Kagame au Ligi Kuu Bara pekee. Azam hii inatakiwa kuanza kujifananisha na timu za Esperance au Etoile du Sahel za Tunisia au TP Mazembe ya Kongo na timu nyingine kubwa Afrika.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe