Wednesday, July 29, 2015



RONALDO? Hapana aisee. Ndivyo ambavyo Kocha wa Manchester United, Louis van Gaal alivyowakata maini mashabiki wa United ambao bado wanasubiri kwa hamu kuona kama Mreno huyo anaweza kurudi Old Trafford.
Van Gaal amekiri kwamba bado anatafuta mshambuliaji staa kuongoza safu ya ushambuliaji Old Trafford, lakini staa huyo hatakuwa Cristiano Ronaldo tofauti na baadhi ya fikra za mashabiki ambao waliamini kuwa Van Gaal angeweza kufanya uhamisho wa kushtukiza kumrudisha Ronaldo.
“Barcelona ina Messi, Neymar na Suarez. Tunahitaji mchezaji wa aina hiyo,” alisema Van Gaal, ambaye inadaiwa kuwa anakaribia kumchukua mshambuliaji wa Barcelona, Pedro kwa dau la Pauni 22 milioni.
Kuhusu dili la Ronaldo, Van Gaal alijibu “Hilo haliwezekani kwa sababu kuna klabu, Ronaldo, pia kuna Manchester United na kiasi gani ambacho Manchester United inataka kutumia,” alijibu kifalsafa kocha huyo raia wa Uholanzi.
Mashabiki wa Man United wamekuwa wakiendelea kumuota Ronaldo ambaye aliichezea klabu hiyo kwa miaka sita chini ya utawala wa Sir Alex Ferguson baada ya kununuliwa kwa Pauni 12 milioni kutoka Sporting Lisbon mwaka 2003.
Hata hivyo, Agosti 2009 aliuzwa kwa dau la Pauni 80 milioni kwenda Real Madrid, ikiwa ni dau la rekodi ya uhamisho wa dunia wakati huo, kabla ya Gareth Bale hajanunuliwa kwa Pauni 85 milioni kwenda Santiago Bernabeu miaka miwili iliyopita.
Wakati Van Gaal akiachana na mpango wa kumchukua Ronaldo, winga wake, Angel Di Maria amepaa mpaka katika Jiji la New Jersey kwa ajili ya kupimwa afya na kukamilisha uhamisho wa Pauni 45.9 milioni kwenda PSG ambayo ipo ziarani nchini humo.
Staa huyo ameamua kujiunga na PSG baada ya kuchemsha katika msimu wake wa kwanza Manchester United ambayo ilimnunua kwa dau la Pauni 59 milioni Agosti mwaka jana kutoka Real Madrid.
Hata hivyo, staa huyo wa kimataifa wa Argentina hatacheza katika pambano la kirafiki kati ya United na PSG ambalo linatazamiwa kufanyika wikiendi ijayo.
Kocha Louis van Gaal amekiri kwamba staa huyo anakaribia kuhama Old Trafford.
Pamoja na kuondoka kwa Di Maria, Van Gaal amefanya uhamisho wa nguvu kwa kuwanunua mastaa sita klabuni hapo huku juzi akikamilisha kumchukua kipa namba moja wa Argentina, Sergio Romero ambaye alikuwa mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na Sampdoria ya Italia.
Wachezaji wengine walionunuliwa na Van Gaal ni Bastian Schweinsteiger (Bayern Munich), Memphis Depay (PSV), Morgan Schneiderlin (Southampton) na Matteo Darmian (Torino).

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe