Wednesday, July 29, 2015



MABAO manne aliyofunga kwenye hatua ya makundi ya michuano ya Kombe la Kagame anayoshiriki kwa mara ya kwanza yamemweka straika Michael Olunga matawi ya juu.
Olunga anayeichezea Gor Mahia ya Kenya ndiye mchezaji aliyepo kwenye vinywa vya mashabiki wengi wa soka wanaofuatilia michuano hiyo ya Kagame. Achana na kuhusishwa kwake na klabu za Simba na Yanga zinazodaiwa kumpigia jaramba ili kumnyakua, lakini umahiri wake uwanjani na hasa katika kufumania nyavu kumemfanya awasisimue wengi. Mkenya huyo amejaliwa nguvu, mbio, chenga na akili ya kucheza soka mbali na pua za kunusa mahali nyavu zilipo.
Mwanaspoti lilibahatika kufanya mahojiano na Olunga na kuweka mambo mengi hadharani na kiu yake ya kuona anafika mbali katika kucheza soka na hamu ya kutwaa Kiatu cha Dhahabu cha michuano ya Kombe la Kagame inayoingia hatua na robo fainali kuanzia leo Jumanne.
Kombe la Kagame
Hii ni mara yake ya kwanza kushiriki michuano hiyo, lakini hata anafurahishwa na kasi aliyoingia nayo kiasi cha kumfanya awe gumzo kubwa kwa mashabiki wa Bongo.
“Tumekuja hapa tukiwa na lengo moja, hili lipo kwa wachezaji wote wa timu yangu, kwamba tujitume timu ipate mafanikio makubwa, tunajua kwamba kila timu iliyokuja hapa ni bora.
“Ninashukuru tunakwenda vizuri na kwa upande wangu nina kiwango ambacho hata mwenyewe kinanifurahisha. Lakini sijaridhika, nimepanga kuongeza bidii zaidi kwani nataka kupata mafanikio makubwa, hii ni vita lazima tupambane,” anasema Olunga.
Kujiuza
Michuano ya Kombe la Kagame imekuwa ikitumiwa na wachezaji wengi kujiweka sokoni na klabu kuingia kwenye vita ya kusaka wachezaji, hasa kwa klabu za Ligi Kuu ya Tanzania Bara kama Yanga, Simba na Azam.
Klabu hizo zimekuwa zikitajwa kumwinda Olunga na kuahidi kumng’oa katika klabu yake ya Gor Mahia anayoichezea kwa msimu wa kwanza.
Hata hivyo, Olunga mwenyewe anasema klabu hizo zinazomsaka ni kama zinajisumbua tu, kwa sababu hana mpango wa kuachana na Gor Mahia maarufu kwa jina la Kagalo kwa hivi sasa.
“Sijapata ofa yoyote kutoka timu hizo, hakuna aliyenifuata, hata hivyo, siwezi kulizungumza zaidi suala hilo kwani nina mipango yangu, kwanza nataka kuisadia timu yangu itwae taji la Kagame na Ligi Kuu Kenya (KPL),” alisema.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe