Wednesday, May 28, 2014


Wachezaji wa timu ya Yanga wakishangilia wakati wa msimu wa ligi kuu uliopita 

DAKTARI wa Yanga, Juma Sufiani amewaasa wachezaji wa timu hiyo kujiepusha na vitendo vya ulevi katika kipindi hiki cha mapumziko na atakayekiuka ataona matokeo yake uwanjani msimu ujao.
“Wachezaji wanatakiwa kujiweka mbali na matumizi ya vitu kama pombe kwa kipindi hiki, wasijiachie sana kwasababu ni mapumziko bali wazingatie kupata mlo mzuri na kufanya mazoezi mepesi kwani hivyo ndivyo vitakavyowajenga.
“Ni jukumu la mchezaji mwenyewe kuielewa kazi yake na kufuata yale tunayowaasa, kazi yetu kama madaktari ni kuwaelimisha wao kufuata mambo yatakayowajenga, hatuwezi kuwafuatilia hata kwa kipindi walichokuwa kambini tuliacha jukumu hilo kuwa lao,” alisema Sufiani
Kwa upande mwingine Daktari wa Simba, Yassin Gembe amewataka wachezaji kuhakikisha wanapata mazoezi yasiyopungua muda wa wiki sita kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa ligi ili kujiepusha na hatari ya kupata majeraha yasiyo ya lazima.
“Kitaalam mazoezi ya wiki zisizopungua sita ni ya lazima kwa mchezaji kabla ya kuanza kwa msimu mpya, wengi wanachelewa kambini na kushindwa kufanya mazoezi kwa kipindi cha muda huu unaotakiwa hivyo kujiweka hatarini kupata majeraha wakati ligi itakapoanza kutimua vumbi,” alisema Gembe.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe