Wednesday, May 28, 2014


Jaji Mstaafu Damian Lubuva


Dar es Salaam.  Serikali imeeleza nia yake ya kufanya maboresho kwenye Daftari la Wapigakura katika mwaka huu wa fedha 2014/15, ikitumia mfumo wa biometric ambao, hata hivyo, unalalamikiwa na vyama vya upinzani nchini.
Uamuzi huo wa Serikali unafanyika ikiwa imepita miaka mitano tangu daftari hilo liboreshwe kwa mara ya mwisho Machi 2009. Hii ni kabla ya kufanyika kwa uchanguzi mkuu mwaka 2010 wakati kambi ya upinzani bungeni ilipoeleza wazi kutilia shaka mfumo huo.
Kwa upande wake, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imepanga kuboresha daftari hilo kwa awamu mbili kwa mfumo huo wa bionetric ili kuondoa kasoro zilizojitokeza katika mfumo wa awali wa Optical Mark Recognition(OMR).
Msimamo wa NEC
Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mstaafu Damian Lubuva anasema lengo la tume hiyo ni kuhakikisha uboreshaji wa daftari huo kwa awamu ya kwanza unakamilika, ili kuwawezesha watu wengi zaidi kushiriki katika mchakato wa kura ya maoni.
Anasema Jaji Lubuva kuwa mfumo wa biometric ambao wanatarajia kuutumia una uwezo wa kumtambua mpigakura kwa alama za mwili, ikiwamo alama za vidole au mboni ya jicho, lengo likiwa ni kuhakikisha uandikishaji unafanyika kwa kiwango ambacho kitaondoa malalamiko au maswali kutoka kwa wadau. 
Jaji Lubuva anasema awamu ya kwanza itafanyika Septemba hadi Desemba, kwa kuandikisha watu wote upya, pamoja na watakaotimiza umri wa kupiga kura yaani miaka 18 katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwakani.
Awamu ya pili inatarajiwa kufanyika kati ya Aprili hadi Agosti mwakani na wapigakura waliohama kutoka sehemu moja kwenda nyingine nchini watapata fursa ya kurekebisha taarifa zao.
Awamu hii  ya maboresho pia inatarajiwa kuwaondoa wapigakura waliofariki au kupoteza sifa na wapigakura wakiwamo watakaokuwa wamepoteza kadi au kadi zao kuharibika.
Tayari, imethibitika kwamba  Serikali imetoa Sh39 bilioni mpaka sasa kwa maandalizi mbalimbali ya uboreshaji kwa awamu ya kwanza, pamoja na kununua vifaa vya kuandikishia.
Jaji Lubuva anasema NEC inatarajia kuanza vikao na wadau mbalimbali ambavyo vitajulisha jinsi mchakato huo wa uboreshaji awamu ya kwanza utakavyoendeshwa  na teknolojia itakayotumika. 
Anasema wako katika hatua za mwisho za ununuzi wa vifaa mbalimbali vitakavyotumika katika uboreshaji huo ili kuhakikisha mchakato huo utakapoanza unakuwa katika hali ya ufanisi zaidi.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe