Wednesday, May 21, 2014



AMSTERDAM, UHOLANZI
VITA inaweza kuzuka Old Trafford kama kocha mtarajiwa wa Manchester United, Louis van Gaal, atafanya kile ambacho kinatabiriwa na wengi klabuni hapo. Kumpa kitambaa cha unahodha Mdachi mwenzake, Robin Van Persie.
Juzi Jumapili, Van Gaal alionyesha kila dalili kwamba Van Persie atakuwa nahodha wake mpya Old Trafford baada ya Nemanja Vidic kutangaza rasmi kuondoka klabuni hapo kwenda Inter Milan msimu ujao.
Van Gaal alimsifu vilivyo Van Persie kwa kudai kwamba ni nahodha wake ambaye wanaendana katika falsafa. Kama atamchagua Van Persie huenda kukatokea mzozo mkubwa kutoka kwa Wayne Rooney ambaye anaamini anastahili kuvaa kitambaa hicho baada ya kuwa klabuni hapo kwa muda mrefu kuliko Van Persie ambaye amehamia hivi karibuni.
“Van Persie ni nahodha wangu, ni mfungaji wangu bora  kwa mwaka mmoja na nusu ambao amecheza chini yangu,” alisema van Gaal mara baada ya pambano la kirafiki dhidi ya Ecuador ambapo Van Persie alisawazisha katika sare ya 1-1.
“Amekuwa mfungaji bora wa muda wote wa timu ya Uholanzi, anacheza soka la uhakika na hata baada ya kurudi kutoka katika kuwa majeruhi, amefunga bao murua. Nimefurahishwa na kiwango chake, lakini pia ni bonge la nahodha.
“Nadhani unamfanya mchezaji awe nahodha wako wakati mnapoendana katika falsafa na morali. Si tu suala la soka na mbinu na kinachotokea uwanjani, bali katika maisha vile vile. Nadhani hilo ni muhimu na naamini kuwa Van Persie na Van Gaal wako katika falsafa moja.”
Van Persie amekuwa nahodha wa Uholanzi kwa kipindi cha miezi 18 iliyopita na kwa sasa yupo katika kambi ya timu ya taifa ya Uholanzi akijiandaa kukiongoza kikosi hicho katika safari ya Brazil kucheza fainali za Kombe la Dunia.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe