Wednesday, May 21, 2014


Kocha wa Mbeya City. 

MEI 22, mwaka huu Mbeya City itaanza harakati zake za kuwania Kombe la Nile Basin linaloandaliwa na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) kwa kushirikiana na Serikali ya Misri.
Jina kamili la michuano hii ni ‘Cecafa Nile Basin Cup’ yaani Kombe la Cecafa la Bonde la Mto Nile. Bendera ya Tanzania itapeperushwa na Mbeya City, timu ngeni kabisa katika soka la ushindani Tanzania lakini imeonyesha ukomavu mkubwa.
Wakati Ligi Kuu Bara inaanza Septemba mwaka jana, hakuna aliyewaza kama Mbeya City ingeweza kuwa moja kati ya timu kali na tishio katika soka la Tanzania. Labda viongozi wa timu hiyo na benchi la ufundi ndio waliowaza makali ya timu yao.
Timu hii imeonyesha kwamba, katika soka lolote linawezekana inapokuwepo nia na malengo ya kutaka kufanikiwa, kinyume cha hapo hakuna litakalotendeka na hakuna njia ya mkato.
Kutokana na uhodari wake, Mbeya City almanusura ishike nafasi ya pili katika ligi lakini ikaishia nafasi ya tatu huku ikipata matokeo mazuri katika mechi 26 za ligi ilizocheza.
Nidhamu ya wachezaji, kocha, viongozi hata mashabiki ndicho kitu pekee kilichoifanya Mbeya City leo hii ipate heshima kokote inakopita nchini. Heshima ya timu hii, imeziongezea thamani jezi zake ambazo zimetapakaa kote nchini.
Sasa Mbeya City imepata nafasi ya kuiwakilisha nchi ndani ya msimu mmoja tu, hizi ni hatua za haraka sana katika ukuaji lakini lazima tukubali kuwa timu hii inapata inachostahili.
Tunaiamini Mbeya City kwamba itafanya vizuri katika michuano hiyo ndio maana hakuna minong’ono yoyote pindi Cecafa ilipoipa nafasi ya kuiwakilisha nchi baada ya Azam FC kutokuwa na nafasi ya kucheza michuano hiyo.
Wote tupo nyuma ya Mbeya City katika kuhakikisha Bendera ya Tanzania inapepea vizuri katika michuano hiyo kwani ushindi wa timu hiyo ni wetu sote, wala siyo wa watu wa Mbeya na vitongoji vyake.
Jukumu la kuiunga mkono timu hii ni letu sote na kamwe hatuwezi kuiacha Mbeya City ikiwa mpweke katika michuano hiyo ukizingatia uchanga wake katika soka la ushindani, tena ngazi ya kimataifa.
Pia, hiki ni kipimo tosha kwa wachezaji wa Mbeya City ambao wanacheza mechi za kwanza za michuano nje ya ardhi ya Tanzania na watambue hiyo ni nafasi yao ya kipekee kujitangaza na kuuza vipaji vyao kimataifa.
Misri ni miongoni mwa nchi chache za Afrika ambazo ligi yake imepiga hatua ikiwa na ufadhili mkubwa unaowezesha wachezaji wake kulipwa mamilioni ya fedha.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe