
Hussein Jumbe akiwa kazini
Ni huzuni. Kumbi za muziki wa dansi ziko tupu. Bendi maarufu
karibu zote zilizotamba miaka ya 70 na 90 zimebaki kuwa historia. Chache
zilizokuwapo tunashuhudia wanamuziki wake wakipigia viti vitupu katika
baa za kawaida kabisa, zilizopo pembezoni mwa jiji la Dar es salaam.
Nini kimetokea kwa muziki huu ambao unabakia kuwa
alama pekee na miongoni mwa burudani ambazo Watanzania wana kila sababu
ya kujivunia, kutokana na historia kuonyesha kuwa muziki huo uliasisiwa
nchini Tanzania na ulianzishwa katika Jiji la Dar es Salaam zaidi ya
miaka 80 iliyopita.
Kati ya wanamuziki wakongwe nchini, Hussein Jumbe
aliyewahi kupigia bendi za Msondo Ngoma na DDC Mlimani Park anapingana
na wanamuziki wenzake wanaoamini kuwa muziki huo unaangushwa na vyombo
vya habari.
Mfano wa kuigwa kuonyesha kuwa muziki huo bado
unakubalika, ni kile alichokifanya Jumbe, akiwa na bendi yake ya Talent
wiki iliyopita katika Ukumbi wa Kisumba zamani Sugar Ray uliopo maeneo
ya Temeke.
Jumbe alifanya uzinduzi wa albamu ya ‘Kiapo Mara
Tatu’, lakini akafanya maandalizi kama ambavyo wanafanya wanamuziki wa
sasa kama vile Jahazi Modern Taarabu, Twanga Pepete, Linah Sanga,
Diamond Plutnamz kwa kualika watu wengine wenye mvuto wanapokuwa
wanazindua albamu zao.
Kama ilivyo kawaida yake, Jumbe licha ya kuwa ni
mwanamuziki wa zamani aliachana na uzamani na kuonyesha kuwa kulialia
kwamba wanamuziki wa zamani hawasaidiwi siyo dawa.
Lakini kitu kilichofanya shoo hiyo ivutie zaidi na
kujiweka katika soko la muziki kama wafanyavyo wanamuziki wengine,
aliweka burudani tofauti tofauti ikiwamo kikundi cha muziki wa asili cha
Hayahaya Ngoma Afrika kutoka Kijiji cha Makumbusho, jijini Dar es
Salaam. Kama hiyo haitoshi katika kuwavutia mashabiki wa muziki wa aina
zote, hakuwatenga wadau wa taarabu kwani mwanamuziki wa miondoko hiyo
Isha Mashauzi alikuwapo kuwakilisha.
Cha kufurahisha ni kwamba Isha Mashauzi, akiwa na
kundi zima la Mashauzi Classic hakumuangusha kwani walifanya kile
mashabiki walichokuwa wanakikusudia, ikiwamo kuimba muziki wa taarabu
kwa ustadi mkubwa na kuimba nyimbo za wanamuziki wa muziki wa kizazi
kipya ikiwamo wimbo ‘Maneno maneno’, wa mwanamuziki Ben Pol na kuuimba
kwa ustadi mkubwa. Pia wimbo wa Injili wa mwanamuziki Bahati Bukuku‘
uitwao ‘Waraka wa Amani’ na nyimbo mbili za mwanamuziki Jumbe ambazo ni
‘nachechemea na ‘siri ya nini’.
Jumbe anena
Mwanamuziki huyo mkongwe alisema kuwa
alichokifanya ni kusoma mahitaji ya soko la muziki wa sasa na kujua
mahitaji ya wadau wa burudani na hatimaye hadi leo anapiga muziki na ana
mashabiki vijana kwa wazee. “Niliwahi kusema kulalamika siyo dawa,
tulijisahau miaka ya 80-90, tulijisahau na vijana wamechukua nafasi
wanaifanyia kazi. Tunachotakiwa kufanya sasa ni kuhakikisha tunaurudisha
muziki wa dansi kwenye chati ingawa kazi kubwa inatakiwa kufanyika,
”anasema Jumbe.
Jumbe anafafanua kuwa licha ya vyombo vya habari
kuusahau muziki huo na wanamuziki wenyewe wanataka ujiuze kwa umaarufu
wa zamani bila kujali dunia inazunguka na inakwenda sambamba na
mabadiliko.“Hata Serikali imefanya mabadiliko, kulikuwa na Chama kimoja
na sasa ni vyama vingi na muziki vivyo hivyo unatakiwa uende na kasi ya
mabadiliko, ”anasisitiza Jumbe.
Jumbe ambaye wimbo wake wa ‘Kiapo Mara Tatu, ambao
ndiyo umebeba jina la albamu hiyo, uliingia kwenye kinyang’anyiro cha
tuzo za Kilimanjaro Music, katika kipengele cha Wimbo bora wa Kiswahili,
ingawa haukufanikiwa kupata tuzo hiyo.
0 comments:
Post a Comment