Monday, May 5, 2014

Kocha Yanga azuia manoti ya usajili wa Mbuyu Twite

 

Mbuyu Twite.

INAWEZA ikawa ahueni au pigo kwa Yanga, kwani Kocha wa Yanga Hans Pluijm amesema kuanzia sasa hakuna mchezaji atakayelipwa fedha zote za usajili wakati viongozi wakifikiria jinsi ya kumalizana na beki wake Mbuyu Twite aliyetaka apewe chake chote.
Pluijm raia wa Uholanzi ameamua kuweka mfumo huo kutokana na usumbufu wa wanasoka wa Afrika kutokana na uzoefu wake, hivyo ameagiza kuanzia sasa usajili wowote utakaofanywa na klabu yake lazima mchezaji alipwe nusu au sehemu ya fedha za usajili tu.
Akizungumza na Mwanaspoti, Pluijm alisema amekutana na mabosi wa Yanga ambao walitaka maoni yake hasa katika kipindi hiki cha usajili na amewaambia mkakati wake huo utakaonusuru fedha za klabu kwa wachezaji wasiowajibika ipasavyo.
Kocha huyo alifafanua kuwa katika mambo aliyoyapinga ni wachezaji kupewa fedha zao zote za usajili wakati wakianza mwaka wao wa kwanza wa ajira.
Pluijm alisema kwa uzoefu wake wa miaka 10 katika kufundisha klabu za Afrika amegundua usumbufu mkubwa wa wachezaji baada ya kupewa fedha zote za usajili mwaka wa kwanza na hivyo hataki kuona usumbufu wa aina hiyo unatokea wakati wa utawala wake.
Kocha huyo ana uzoefu wa kufundisha soka la Afrika kwa miaka zaidi ya 10 akiwa amewahi kufanya kazi kwa vipindi tofauti na klabu za Ghana za Medeama SC, Berekum Chelsea, Heart of Lions Kpando na Ashanti Gold SC.
Pluijm alisema pia amesikia taarifa za Twite anayetaka kupewa fedha zote, kwanza akakiri kuwa bado anamuhitaji mkongwe huyo ingawa  akaagiza nyota wote watakaosajiliwa kuanzia sasa wasipewe fedha zao zote wakati yeye akiwa kocha Yanga.
Hata hivyo kocha huyo amewataka mabosi wa Yanga kuheshimu ahadi za kumalizana na wachezaji haraka katika mwaka wao wa pili unapoanza ili yasiwepo malalamiko kuhusu malipo jambo alilosema linapoteza ufanisi wa wachezaji katika timu.
“Nimewaambia viongozi kuwa sikubaliani na suala la mchezaji kupewa fedha zote mwaka wa kwanza wa usajili, kama wakiingia mkataba na mchezaji yeyote mfano uwe wa miaka miwili basi wampe nusu ya fedha, zinazobaki apewe katika mwaka wake wa pili wa mkataba,”alisema Pluijm.
“Nawajua wachezaji wa Afrika, ni wasumbufu katika mwaka wao wa pili baada ya kumaliza fedha endapo utampatia zote, ukiacha hilo pia nimewaambia kuhusu kuheshimu makubaliano, wahakikishe wanamalizana na wachezaji kwa wakati si kuwapiga chenga,”alisema.
Kama uongozi wa Yanga utaheshimu agizo hilo, huenda Emanuel Okwi akaathirika kwani alisajiliwa kwa dola 100,000 hivi karibuni na anaidai timu hiyo salio lake la dola 40,000 ndio maana akasusa kucheza mechi za mwisho za msimu uliopita.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe