Tuesday, April 29, 2014

TFF yashikilia usajili wa Twite, Kavumbagu Yanga

KUNA kasheshe moja linanukia kwenye usajili mpya. Ni kasheshe  ambalo Simba huenda wakachekelea kwa vile linaweza kuleta athari kwa watani wao wa jadi, Yanga. Tayari kocha wa Jangwani, Hans Pluijm, ameshakosa raha na anakuna kichwa.
Kwa mujibu wa azimio la Bagamoyo ambalo lilikubalika na klabu zote za Ligi Kuu Bara kwamba lianze kutumika msimu ujao, klabu za ligi hiyo zitalazimika kupunguza idadi ya wachezaji wa kigeni kutoka watano mpaka watatu.
Lakini klabu zitapaswa kukutana hivi karibuni kupitisha upya makubaliano hayo ambayo kama Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) likiyakomalia, itakuwa ni hasara kwa Yanga kwani haitakuwa na nafasi ya kuwachomeka wachezaji wake wawili wa kigeni. Didier Kavumbagu wa Burundi na Mbuyu Twite wa Rwanda.
Wachezaji hao mikataba yao imemalizika na kufanya Yanga kusaliwa na wachezaji watatu wa kigeni wenye mikataba ambao ni Emmanuel Okwi na Hamis Kiiza wote wa Uganda pamoja na Haruna Niyonzima wa Rwanda.
Hatma ya Twite na Kavumbagu kuongezewa mikataba itategemea na uamuzi wa kikao cha viongozi wa klabu na TFF kitakachofanyika hivi karibuni kujadiliana mambo mbalimbali likiwemo hilo la usajili wa wachezaji watano wa kigeni.
Pluijm amekiri kwamba bado hajafanya uamuzi kutokana na utata wa idadi ya wachezaji wa kigeni.
Simba huenda isiathirike kama makubaliano hayo yatapita kwani imepanga kumchomoa kipa Mghana, Yaw Berko kwenye usajili wake na kumsajili kipa wa Yanga, Ally Mustapha 'Barthez'.
Hivyo Simba itakuwa imesaliwa na wageni watatu ambao ni mabeki Donald Mosoti (Kenya), Joseph Owino (Uganda) na straika Amissi Tambwe wa Burundi.
Azam yenyewe ina wachezaji wanne wa kigeni, Kipre Tchetche, Kipre Bolou na Mohammed Kone wote wa Ivory Coast na Brian Umony wa Uganda.
Akizungumza hilo, Kavumbagu aliyemaliza msimu akiwa na mabao 13, alisema: "Mimi siwezi kukaa muda wote huo nikisubiria kanuni hizo mpya za usajili, kama wananihitaji wanipe mkataba nisaini, kikubwa wanachotakiwa kutambua kuwa soka ndiyo ajira yangu.
"Nipo tayari kuichezea timu yoyote ile inayohitaji, hata JKT Ruvu wenyewe wakinihitaji wanifuate kwa ajili ya mazungumzo kwa masharti maalumu nitakayohitaji kwenye mkataba wangu."
Alipoulizwa kuhusiana na suala hilo, Katibu Mkuu wa TFF, Selestine Mwesigwa, alisema: "Klabu zinatakiwa kuwa makini katika kipindi hiki cha usajili kwa ajili ya msimu ujao, kikubwa zinatakiwa kufuata kanuni za usajili."

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe