Siku ya kukumbukwa Muungano

Komandoo wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), akiwa ameruka kwa miguu yote hewani na kuvunja mbao zilizokuwa zimeshikwa na wenzake wakati wa maonyesho ya kijeshi ya Maadhimisho ya Miaka 50 ya Muungano kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam jana. Picha na Emmanuel Herman
Dar es Salaam. Makomandoo wa Jeshi la Wananchi
wa Tanzania (JWTZ) jana walizipamba sherehe za maadhimisho ya miaka 50
ya Muungano, baada ya kuonyesha umahiri wa mapigano ya kujihami dhidi ya
maadui kwa kutumia viungo vyao, huku baadhi ya askari wengine wakirusha
ndege za kivita na kuruka na miamvuli (Parachute).
Unaweza kusema maelfu ya wananchi waliohudhuria
maadhimisho hayo yaliyofanyika katika Uwanja wa Uhuru jana walikuwa
wakiwasubiri wanajeshi hao, kwani baada ya kutambulishwa na Meja Evans
Mtambi, wananchi hao walianza kuwashangilia kwa nguvu.
Makomando wenye miili ya ukakamavu waliingia
katika uwanja huo saa 4:43 asubuhi wakiwa katika makundi matatu katika
siku hiyo ambayo ni ya kukumbukwa.
Yalianza kuingia makundi mawili kwa mwendo wa
kurukaruka kwa ukakamavu, huku wakitoa salamu ya utii kwa Rais Jakaya
Kikwete, kitendo kilichozidisha shangwe uwanjani hapo.
Mara baada ya kupita kwa makundi hayo, liliingia
kundi la tatu likiwa na makomandoo 18, ambapo 17 kati yao walikuwa
wamevalia fulana nyeusi na suruali za kijeshi, huku kiunoni wakiwa
wamening’iniza ala ya kuhifadhia kisu.
Walianza kwa kuonyesha mitindo mbalimbali ya
kujihami na adui kwa kutumia viungo vyao, fimbo na visu huku wakijirusha
hewani na kutua chini kwa mtindo wa aina yake.
Katika hali isiyotarajiwa, wanajeshi hao walianza
kuvunja matofali kwa kutumia ngumi na kichwa, kitendo kilichowafanya
wananchi na wageni mbalimbali waliohudhuria maadhimisho kuwashangaa kwa
uhodari huo.
Wakiwa hawaamini wanachokiona, ghafla mmoja wa
wanajeshi hao alilala chali na kupangiwa matofali mawili makubwa
tumboni, ambayo yalivunjwa na mwenzake aliyetumia nyundo kubwa.
Huku baadhi yao wakiwa wamevua fulana na kubaki vifua wazi, walianza kuchapana kwa kutumia mbao ngumu katika miili yao.
Kila mbao hizo zilipokuwa zikitua katika miili ya
wanajeshi hao, zilikuwa zikipasuka vipandevipande mithili ya ubao
uliokanyagwa na lori la mizigo.
Kuruka kwa miamvuli
Kivutio kingine kilikuwa ni wanajeshi watano
walioruka kwa miamvuli (Parachute) kutoka umbali wa futi 4,500 kutoka
usawa wa bahari huku wakielekezwa jinsi ya kutua na moshi wa kijani
ambao husambaa hewani kwa kufuata uelekeo wa upepo.
0 comments:
Post a Comment