Friday, April 18, 2014

KUTOKA LONDON: Athari za anguko la Manchester United

 

LIGI Kuu England inaelekea ukingoni na  ndoto za mabingwa watetezi, Manchester United za kuendelea kubaki na kombe hilo zimepeperuka baada ya kushuhudia vipigo vingi, hasa nyumbani kwao, Old Trafford.
Huu ni uwanja ambao katika miaka mingi ya kocha Sir Alex Ferguson ilikuwa ngome inayoogopwa na wachezaji na makocha wa timu pinzani, lakini tangu msimu huu umeanza wakiwa chini ya David Moyes, mambo yamegeuka.
Man United imekuwa timu ya kubezwa, ambayo imefungwa na timu nyingi ndogo, baadhi ikiwa ni mara ya kwanza katika historia zao kuwafunga Mashetani Wekundu, mfano Swansea.
Rekodi nyingi zimewekwa na kuvunjwa, lakini kwa upande hasi kwa United ambao sasa wanajaribu kujitutumua ili walau wacheze Ligi ya Europa japokuwa vigingi mbele yao bado ni vingi kwa jinsi timu nyingine zinavyowawekea kauzibe.
Athari za matokeo hayo kisaikolojia zinamuumiza zaidi kocha ambaye aliona ni heshima kubwa sana kupata nafasi ya kuwafundisha mabingwa hao na moja ya klabu zinazoheshimika zaidi duniani.
Lakini matokeo haya naathiri pia chapa ya Ligi Kuu ya England (EPL) machoni pa ulimwengu wa michezo, kwa sababu kimsingi kutetereka huko kunashusha kwa namna fulani hadhi ya ligi yenyewe.
Hii ni kwa sababu  za anguko la Manchester United haziishii ndani tu, bali pia nje ya nchi, kwa sababu kwa mfano kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya (UCL) licha ya kufika hatua ya robo fainali, ilikuwa bahati zaidi kuliko uwezo.
Tunakumbuka bado jinsi Olympiakos walivyowaadhiri kwenye mchezo wa kwanza na kuwafunga 2-0, timu ambayo ni ndogo ikilinganishwa na United. Lakini pia mchezo dhidi ya Bayern Munich ambapo United walilazimisha sare, ‘waliegesha basi’ ndiyo maana winga wa Wajerumani hao, Arjen Robben akasema ilikuwa kana kwamba United wanajihami kwenye mpira wa mikono.
Mtaalamu wa masuala ya soka na biashara kuhusiana na chapa na matangazo, Evans Brighton anasema kwamba hii ni sawa na panga lenye kukata kuwili kwa sababu klabu kubwa kama hii inapoanza kufanya mambo ya  ovyo, inapunguza washabiki kwenye ligi husika na kidogokidogo mapato.
Hii ni timu iliyopata kutwaa ubingwa wa England mara 20, ikawa na kocha aliyesifika kote duniani na kuna watu waliokuwa wakiweka fedha zao kwenye ligi hii kwa sababu ya timu, kocha wake, aina ya wachezaji waliopo au hata wamiliki kwa maana ya uhakika wa kufanya vyema.
Lakini moja ya klabu kubwa kama hii inapodondoka tafsiri yake kimataifa ni kwamba na utamu wa ligi unaweza pia kuwa na tatizo, watu wakaamua kuelekeza macho yao kwenye ligi nyingine.
Ikumbukwe kwamba Ligi Kuu England ndiyo sasa maarufu zaidi kote duniani, lakini kadiri miaka inavyokwenda watu wanakuja na hoja kinzani, wakianza kutupia macho Bundesliga (Ligi Kuu Ujerumani), La Liga (Ligi Kuu Hispania) na hata Ligue 1 (Ligi Kuu Ufaransa)

 




0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe