Friday, April 18, 2014

Buriani Kamanda Muhidin Gurumo

 

Sijui niseme nini, sijui nilie, lakini Napata shaka hakuna atakayenielewa kwa vijana wengi ambao wamenizunguka hapa nilipo hawafahamu thamani ya mwanamuziki nguli  Muhidin Mwalimu Mohammed Gurumo maarufu Kamanda, ambaye amefariki dunia.
Sitaki kuamini ninachokisikia kutokana na baraka nilizozipata kwa nguli huyu, ikiwemo tuzo kwa kuandika makala zake, kumtambulisha kwa mara nyingine kwenye jamii baada ya kujitambulisha mwenyewe kupitia muziki wake aliouimba kwa ustadi mkubwa, lakini heshima, uthamini na kujali alipokuwa akinipa pindi ninapomtembelea nyumbani kwake.
Lakini sitasahau alipokuwa akifanya mazoezi Jumamosi kadhaa na kuja hadi ofisini kunisalimia.
Mara nyingi alikuwa mcheshi na mwenye utashi, namnukuu, “Waandishi wengi wamekuwa wakinihoji, lakini Mwananchi mna utashi mkubwa na mahojiano yenu yanayoendelea nami yananifanya nipate watu wapya wanaonifahamu na kunikumbuka ambao walinisahau kabisa ikiwemo Serikali,”alisema Gurumo akinisindikiza kutoka nyumbani kwake Makuburi hadi kituo cha mabasi cha Gereji, ambako nilipanda gari na kurudi ofisini.
Binafsi napata ukakasi kuandika makala haya, lakini nakiri kuwa hakuna jinsi zaidi ya kukubali alichokifanya Mungu kwa kuwa kazi yake haina makosa, kabla ya kuendelea nasema  “Pumzika kwa amani kipenzi, Muhidini Mwalimu Gurumo.
Namfahamu Gurumo kutokana na kuwa mpenzi wa muziki wa wa zamani, lakini kukutana naye na kuzungumza naye kirefu ilikuwa ni mwaka jana, nilipomtembelea  nyumbani kwake Ubungo Makuburi, jijini  Dar es Salaam.
Lengo la safari yangu ilikuwa ni kufahamu hali yake baada ya kupata taarifa za kuumwa kwake  na kulazwa katika wodi ya wagonjwa mahututi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Baada ya kuugua kwa muda mrefu ugonjwa wa moyo na mapafu, lakini pia nilienda kuchota hazina ya historia ya maisha yake ya muziki.
Gurumo alikuwa mcheshi na mwenye  moyo wa kunifahamisha yeye ni nani na alitoka wapi na anafahamu nini kuhusu muziki wa dansi.
Nikiwa kwake, tulizungumza mambo mengi ambayo yalinifanya niandike makala kadhaa za kuvutia kumuhusu mwanamuziki huyu nguli, moja ya malalamiko yake ilikuwa ni kuimba muziki kwa miaka kadhaa bila mafanikio, lakini akanidokeza lengo lake la kustaafu muziki kutokana na afya yake kutokuwa nzuri na umri kuwa mkubwa.
Gurumo (74), alitangaza uamuzi wake wa kustaafu muziki Agosti 22, mwaka 2013 ,  alipozungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Idara ya Habari (Maelezo), jijini  Dar es Salaam.
Wakati huo alizungumza mambo mengi na mojawapo ni kustaafu muziki bila kuwa na kitu chochote cha maana hata baiskeli licha ya kuimba kwa zaidi ya miaka 50.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe