Sunday, March 9, 2014

STERLING: Mjamaica aliyeanza kuikamata England

        

                  Raheem Sterling akishangilia bao na straika  wa  LiverpoolSuarez 

HAKUNA unachoweza kubisha. Huu ni wakati wa mwanasoka, Raheem Sterling, kutamba katika Ligi Kuu England. Ameingilia kombinesheni ya Luis Suarez na Dan Sturridge na sasa anang’ara kuliko zamani. Jikumbushe kuhusu uwepo wake Anfield. Ni nani huyu Sterling?
Azaliwa Jamaica, akulia England
Raheem Shaquille Sterling alizaliwa Desemba 8, 1994 katika mji mkuu wa Jamaica, Kingston. Sterling alikulia katika eneo la Maverley jijini Kingston huku akilelewa na bibi yake. Akiwa na umri wa miaka mitano alihamia London, England pamoja na mama yake.
Alianza maisha yake ya soka la utotoni katika klabu ya Queens Park Rangers, lakini Februari 2010 kocha wa wakati huo wa Liverpool, Rafael Benitez, alimnunua kwa ada ya Pauni 600,000 ambayo ilitazamiwa kupanda hadi Pauni 5 milioni kutegemea na jinsi ambavyo angepiga soka lake kwa uhakika Liverpool.
Alicheza mechi yake ya kwanza ya timu ya wakubwa katika mechi za maandalizi ya msimu dhidi ya Borussia Monchengladbach ya Ujerumani Agosti Mosi, 2010.
Hata hivyo wakati huo alikuwa bado akiendelea kutisha katika timu ya vijana kutokana na kasi yake huku akifunga katika mechi za vijana za Hibernian, Aston Villa na kisha katika michuano ya FA dhidi ya Notts County. Februari 14, 2011, Sterling alifunga mabao matano peke yake katika ushindi wa 9–0 dhidi ya Southend United.
Aweka rekodi Anfield
Machi 24, 2012, Sterling aliingia katika pambano dhidi ya Wigan Athletic akiwa na umri wa miaka 17 na siku 107. Kwa kufanya hivyo akawa mchezaji wa pili kinda zaidi kuichezea klabu hiyo. Akacheza tena katika mechi dhidi ya Fulham, kisha katika mechi ya mwisho dhidi ya Chelsea akiingia katika kipindi cha pili ambapo walishinda 4–1.
Agosti 2012 alicheza mechi yake ya kwanza ya Ulaya dhidi ya Gomel wakishinda bao moja. Akafunga bao lake la kwanza timu ya wakubwa katika mechi dhidi ya Bayer Leverkusen katika pambano la kirafiki.
Alianza mechi yake ya kwanza ya Ligi pale Anfield siku tatu baadaye katika sare ya 2–2 dhidi ya Manchester City. Akacheza dakika zote 90 katika kichapo dhidi ya Arsenal Septemba 2 kabla ya kucheza katika sare dhidi ya Sunderland ambapo alipachikwa kuwa Mchezaji Bora wa mechi.
Akasafiri kwenda Europa kucheza dhidi ya Young Boys ya Uswisi akiingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Stewart Downing katika ushindi wa 5–3 wa Liverpool. Bao la kwanza la Sterling lilikuja katika ushindi wa 1-0 dhidi ya Reading. Kwa kufanya hivyo aliweka rekodi ya kuwa mchezaji wa pili kinda zaidi kuifungia Liverpool nyuma ya Michael Owen.
Desemba 21, 2012, Sterling alisaini mkataba mpya na Liverpool. Akafunga bao lake la pili Anfield dhidi ya Sunderland katika ushindi wa 3-0 akinyanyua mpira juu kwa kipa wao wa sasa, Simon Mignolet.
   

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe