Sunday, March 9, 2014

Hakuna Manchester City bila ya mtu huyu

       Yaya Toure 

KUNA kitu unakiona halafu unashusha pumzi. Ndege inatua, ipo katika kasi, rubani anaituliza, halafu dakika chache baadaye inasimama. Unashusha pumzi. Unatafuta mzigo wako ulipo. Ni kama ilivyo unapokuwa kwenye basi au boti.
Ni kama unavyomalizia kusoma mstari wa mwisho wa kitabu cha Sidney Sheldon, James Hadley Chase au John Grisham. Unavuta pumzi na kufunga kitabu huku unatafakari. Ni kama unavyomaliza kutazama filamu ya ‘Sometimes In April’ inayoelezea mauaji ya Rwanda ya mwaka 1994.
Ni kama nilivyotazama shuti la Yaya Toure dhidi ya kipa wa Sunderland, Victor Manonne, Jumapili jioni. Akiwa umbali wa mita 30, alijikunja kiurahisi kama mzaha. Akajikunjua na kuusafirisha mpira mpaka katika kona ya nyavu ya lango lile la Uwanja wa Wembley.
Hakuna kingine unachoweza kufanya. Unashusha pumzi. Binafsi nilishusha pumzi na kutafuta albamu yangu ilipo. Nikatazama picha ambayo nilipiga naye Abidjan Juni 2010. Moyoni nikajisemea ‘Asante Mungu nilikutana na huyu mtu aliyepiga hili shuti na nikazungumza naye’.
Ndiyo Yaya Toure, katika ubora wake wa hali ya juu kabisa kwa sasa ni viungo wachache wanaomudu nguvu zake na akili yake ya soka. Nilikutana naye katika ardhi ya kwao akiwa hana makeke, mpole na msikivu aliyepindukia.
Muda mwingi alionekana kusifia ubora wa mshambuliaji wa Tanzania, Mbwana Samata. Kisha akasifia Taifa Stars ilivyobadilika, tofauti na ile waliyocheza nayo mechi ya kirafiki Januari 2010.
Kinachonifurahisha kwa sasa ni jinsi ambavyo matajiri wa Kiarabu na mashabiki wazungu wa Manchester City hawaiamini timu yao bila ya yeye. Hakuna Manchester City bila ya Yaya Toure. Sahau kuhusu, Kun Aguero, David Silva, Alvaro Negredo na wengineo. Hakuna Man City bila huyu mtu.
Kundi la wachezaji wa Manchester City linapomzunguka kumpa heshima mtu mweusi anayewabeba, basi ni tukio ambalo linaweza kutingisha hata kaburi la Martin Luther King. Ni tukio ambalo linanikumbusha Oktoba 1999 wakati Nwankwo Kanu alipoifunga Chelsea ‘Hat Trick’ katika dimba la Stamford Bridge na mwisho wa mechi wazungu; Dennis Bergkamp na Marc Overmas, wakampelekea taulo ajifute jasho.
Kuna mambo makuu matatu yanayonikosha kuhusu Yaya. Kwanza kabisa ni Mwafrika ambaye hana makeke licha ya mabilioni ya pesa anayokamata. Wanasoka wengi wa Afrika ni mabingwa wa matanuzi baada ya kupokea mishahara mikubwa.
Yaya anapokea Pauni 250,000 kwa wiki. Huwezi kusikia kuwa amenunua gari la kifahari kupindukia, hauwezi kusikia amekodi ndege binafsi kwa ajili ya kwenda likizo Abidjan na wala hauwezi kusikia amenunua saa ya Pauni 2,000.
Lakini jaribu kuangalia makeke ya Emmanuel Adebayor katika maisha yake ya kila siku halafu mlinganishe na Yaya. Kwa sasa Adebayor naye anamiliki ndege yake binafsi kwa ajili ya matanuzi. Usije kudhani kwamba Yaya anaweza kufanya hivyo.
Daniel Amokachi ‘The Bull’ pia akiwa anacheza Uturuki tu katika klabu ya Besiktas, alinunua ndege ndogo. Sasa anajuta. Hata Samuel Eto’o Fills naye anamiliki ndege ndogo. Ndivyo wachezaji wetu wa Kiafrika wanachofikiria kwa haraka zaidi.

 

 

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe