Monday, March 3, 2014

Matajiri Yanga wavamia kambi ya Al-Ahly Cairo

   

Wachezaji wa timu ya Yanga wakishangilia ushindi wa bao moja dhidi ya timu ya Al-Ahly ya Misri.

MATAJIRI wawili wenye ushawishi mkubwa na wanaofanya mambo mengi ya Yanga, hawajaridhika na ushindi wa juzi Jumamosi wa bao 1-0 dhidi ya Al Ahly na sasa wameamua kuivalia njuga klabu hiyo ya Misri kwa kuvamia mji wao wa Cairo ili kuweka mambo sawa kabla ya mechi ya marudiano ya Jumapili.
Wakati jopo la Yanga lilitangulia kuwasili Cairo jana Jumapili  kudhibiti mbinu za Waarabu hao na kuhakikisha hakuna fitna yoyote itakayofanyika, wenyeji wao walikuwa nchini ambapo jioni walifanya mazoezi yao ya mwisho na baadaye kula chakula cha usiku na maofisa wa ubalozi wao nchini na wataondoka leo Jumatatu.
Matajiri hao ambao ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Abdallah Binkleb na Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Kimataifa, Seif Ahmed wamewaongoza wanachama wengine kuingia msituni kuidhibiti Ahly kwa ushirikiano na Watanzania wanaoishi jijini Cairo, Misri.
Seif aliondoka nchini kimyakimya na akaliambia Mwanaspoti kwamba wamepania kuiondosha Ahly na wanachokwenda kufanya ni kuhakikisha Wachezaji wa Yanga wanakuwa chini ya uangalizi mkali katika kila dakika tangu watakapotua kwenye Uwanja wa Ndege Alhamisi wiki hii.
Seif alisisitiza kuwa walishaanza kuweka mazingira mapema, lakini sasa wanakwenda kujidhatiti zaidi kuanzia kwenye Uwanja wa kufanyia mazoezi, hoteli, mabasi pamoja na vyakula kwani hawataki kutumia kitu chochote cha wenyeji ili kuepuka hujuma kwenye mechi hiyo itakayochezwa Jumapili usiku.
“Tumepata ushindi wa kihistoria lakini hatuwezi kukaa chini kushangilia, kwa sasa tunatakiwa kuanza maandalizi ya mechi ya marudiano ndio maana naondoka kuelekea Misri kufanya mambo,” alisisitiza Seif.
“Tunatakiwa kujipanga vizuri kabla ya mchezo wa marudiano, kabla ya timu kufika kuna mambo ambayo ni lazima tuyaweke sawa ili kukamilisha lengo letu la kusonga mbele, kuna haja ya kuandaa sehemu salama ya kufikia kikosi chetu, wapi tutafanyia mazoezi ni lazima tuyafanye hayo yote sasa, hawa jamaa inabidi kuwa nao makini sana.”
Akizungumza na Mwanaspoti, Abdallah Bin Kleb alisema: “Tunajua wenzetu watakuwa wamejiandaa kuhakikisha wanatufunga nyumbani kwao, hivyo tumeanza maandalizi rasmi katika kuhakikisha tunapata ushindi ugenini baada ya kuwafunga nyumbani.
“Kiongozi mmoja anatangulia Misri, timu inaondoka Alhamisi na kufika Ijumaa, itachelewa kuondoka kutokana na mechi hiyo kuchezwa Jumapili.”
Kocha Al Ahly aitisha
Kocha Mkuu wa Al Ahly, Mohamed Youssef, amesema kuwa hatakubali kufungwa mara mbili na Yanga, ugenini na nyumbani.
“Nimeziona mbinu za wapinzani wangu Yanga, sina hofu ya mechi ya marudiano tutakayorudiana na wapinzani wetu, nimepanga kwenda kukiboresha kikosi changu ili mechi ya marudiano tushinde,” alisema.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe