Thursday, February 13, 2014

      Mzungu aipangua first eleven Simba

    

                                      Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic

KOCHA wa Simba, Zdravko Logarusic, ametangaza mabadiliko makubwa katika kikosi chake kitakachoivaa Mbeya City Jumamosi wiki hii.
Amesema ataingiza sura tatu mpya na kubadili uchezaji huku akiwataka mashabiki kutoshituka kwani imebidi iwe hivyo.
Simba haikufanya vizuri katika mechi mbili za ugenini baada ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar mjini Morogoro kisha kulala bao 1-0 mbele ya Mgambo JKT mjini Tanga.
Kwa sasa Simba ipo nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 31 wakati Mbeya City ni ya tatu ikiwa na pointi 34, zote zimecheza mechi 17.
Katika kikosi chake, Logarusic, amewaweka kikosi cha kwanza William Lucian ‘Gallas’, Said Ndemla na Henry Joseph huku akiwaondoa kikosini Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Haruna Shamte na Awadh Juma.
Hivyo kikosi cha sasa cha Simba kitaundwa na Ivo Mapunda, Gallas, Henry, Joseph Owino, Donald Mosoti, Jonas Mkude, Ramadhan Singano ‘Messi’, Ndemla, Amissi Tambwe, Amri Kiemba na Haruna Chanongo.
Katika mazoezi ya timu hiyo yaliyoshuhudiwa na Mwanaspoti, Logarusic, alionekana amepanga kikosi hicho huku akiwapa maelekezo ya kila mara wale walioingia kikosini kwa mara ya kwanza.
Kikosi cha mwisho cha Simba kilichocheza dhidi ya Mgambo kilikuwa; Mapunda, Shamte, Baba Ubaya, Owino, Mosoti, Mkude, Kiemba, Awadh, Messi, Tambwe na Ali Badru.
“Ninachotaka ni ushindi, nitampa nafasi mchezaji ambaye atawajibika ipasavyo uwanjani si zaidi ya hapo, kama umeona mabadiliko hayo ni kweli nimeyafanya kwa manufaa ya timu yangu,” alisema Logarusic ambaye ni raia wa Croatia.
Baba Ubaya sasa anapikwa ili acheze nafasi ya winga wa kulia, wakati kiungo Henry Joseph ataanza kuchezeshwa beki wa kushoto kuanzia wikiendi hii.
Logarusic alikuwa akimwelekeza Baba Ubaya mahali pa kusimama kama winga pia jinsi ya kucheza kwa kusaidia sehemu ya kiungo. Kocha huyo pia alikuwa akimpa maelekezo Henry Joseph aliyechezeshwa beki wa kushoto nyuma ya Haroun Chanongo.
“Issa (Baba Ubaya) nimeona anafaa kucheza winga kuliko beki, ndiyo maana umeona nampa mazoezi ya kucheza nafasi hiyo. Hii ni hali ya kawaida katika timu hasa wakati kama huu tunaotafuta matokeo kwa nguvu, Henry ni mzoefu nataka kutumia uzoefu wake kuipa mafanikio Simba, ataweza kucheza beki hakuna tatizo.”

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe