Thursday, February 13, 2014

                         

                                                          Adamu Mwanakatwe

RAFIKI yangu mmoja, Abdul Nsembo kiutani ana tabia ya kukuhesabia vitu alivyokuzidi maishani. Mwishowe kabisa anakwambia amekuzidi hata dhambi zake. Kwamba anazo nyingi kuliko zako.
Ni kama Wamisri. Wana uwezo mkubwa wa kutuhesabia jinsi walivyotuzidi kwa kila kitu. Uchumi, soka, mipango, historia. Na hata dhambi nazo wametuzidi. Historia yao ya mauaji ya kinyama siku za karibuni yanadhihirisha hilo.
Na hata wakati Al Ahly ya Misri ikijiandaa kucheza na Yanga katika pambano lake la raundi ya kwanza la Ligi ya Mabingwa Afrika, inaonekana kama vile wameizidi Yanga kila kitu. Kuanzia soka lao, uchumi wa klabu na hata dhambi.
Al Alhy wapo hapa jijini Dar es Salaam. Wamejikita katika kuichunguza Yanga. Hata hivyo asilimia 90 ya hali halisi ni kwamba wanapewa nafasi kubwa ya kuitupa Yanga nje ya mashindano. Lakini wameiheshimu Yanga.
Yanga hawajali sana. Wao wapo wapo tu. Furaha yao kubwa katika siku za karibuni ilikuwa ni kuwachapa Mbeya City. Baada ya hapo wakafurahia sare ya watani zao Simba na Mtibwa pale Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
Baada ya hapo wakafurahia ushindi wa mabao 7-0 dhidi ya vibonde Komorozine katika pambano ambalo wachezaji watatu wa Yanga wangeweza kucheza mechi wakiwa wamefumba macho na bado timu yao ingeshinda.
Baada ya hapo Yanga wamejikita katika kufurahia kichapo cha bao 1-0 ambacho watani zao wamepata kutoka kwa Mgambo. Lakini wakati Yanga wakifurahia kichapo cha Simba kwa Mgambo, kocha Msaidizi wa Al Ahly, Ahmed Ayoub na skauti mkuu wa timu hiyo walikuwa Uwanja wa Chamazi kuomba kutumia huduma za kisasa za uwanja huo wakati wa mechi yao dhidi ya Yanga.
Hapa ndipo unapogundua kuwa tunaishi katika dunia mbili tofauti. Mechi ya Yanga na Comoro ni wazi kuwa imeshamalizika. Lakini ni namna gani Yanga wanajiandaa kucheza na Al Alhy? Hauwezi kujua.
Kabla hata Yanga hawajaingiza timu kucheza na Comoro ilikuwa ni wazi kwamba Wacomoro walikuwa wamejifia. Walipaswa kuanza kuichunguza Al Ahly mapema zaidi. Walipaswa kujua timu yao itafikia hoteli gani Cairo, itafanyia mazoezi wapi, na hoteli yao iko umbali gani kutoka uwanjani.
Walipaswa kujua ni timu gani wanaweza kucheza nayo Afrika Kaskazini kabla ya kwenda Cairo.
Sijui kama wamejipanga kwa hili mapema, lakini kwa wenzetu mechi ya soka ina maandalizi ya muda mrefu. Kwa sisi Watanzania utakachoweza kusikia baada ya Yanga kuitoa rasmi Comoro ni kwamba ‘Tunamtafutia kocha mikanda ya Al Ahly’.
Hapo unakuta kocha anatafutiwa mikanda ya Al Ahly ya misimu mitatu nyuma. Unakuta baadhi ya wachezaji wamehama, kocha amebadilika, timu imeingiza wachezaji chipukizi. Na bado unajisifu kuwa umeisoma timu katika mkanda wa video.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe