Friday, February 14, 2014

INAWEZEKANA: Man City wanavyomhitaji kiungo wao Fernandinho

                   

KWA sasa kiungo wa Manchester City, Fernandinho ni majeruhi. Kiungo huyu amekuwa kati ya viungo bora katika Ligi Kuu England msimu huu.
Ni mchezaji muhimu sana katika kikosi cha kwanza cha Manchester City. Manchester City wameshindwa kutamba katika mechi zao mbili za mwisho jambo ambalo limewashangaza mashabiki wengi wa soka hasa wale wa timu hiyo.
Jumamosi iliyopita walitoka sare dhidi ya Norwich na wote tunakumbuka, kwamba walifungwa na Chelsea katika uwanja wao wa nyumbani wiki iliyopita!
Katika mechi hizi mbili, Fernandinho hajacheza kutokana na kuwa majeruhi na ni wazi kwamba pengo lake limedhihirika.
Naamini kocha wa Manchester City, Manuel Pellegrini kushindwa kumpanga Fernandinho kutokana na kuwa majeruhi ni moja ya sababu za Manchester City kupoteza pointi katika mechi za hivi karibuni.
Katika misimu ya karibuni wachambuzi wengi wa soka wanaamini kwamba Yaya Toure ni kiungo bora katika Ligi Kuu England. Ni kutokana na uwezo wake mkubwa wa kushambulia na kukaba. Pia Yaya Toure ana pumzi ya kutisha na huwa anakimbia kutoka 18 ya Manchester City mpaka 18 ya timu pinzani. Hufanya hivyo mara nyingi na katika mechi moja.
Waingereza wanawaita wachezaji kama Yaya Toure “box to box players”- kwa maana ya mchezaji wa kutoka boksi hadi boksi. Kuna wachezaji wachache kama Yaya Toure duniani, lakini, Fernandinho pia ni “box to box player” na mchezo wake unafanana na ule wa Yaya Toure.
Fernandinho pia ana nguvu ya kutisha na tumeona msimu huu kwamba Yaya Toure na Fernandinho wakicheza pamoja kuna timu chache sana ambazo zinaweza kuwafunga Manchester City!
Kwa muda mrefu nimeamini kwamba Manchester City wana kikosi bora katika Ligi Kuu England. Ni kwa kuwa timu hiyo ina zaidi ya mchezaji mmoja mzuri katika kila nafasi.
Kwa mfano, hata kama Sergio Aguero ni majeruhi kwa sasa, kuna washambuliaji wengi wenye uwezo wa kufunga magoli kama Edin Dzeko, Negredo na Jovetic.
Lakini, katika nafasi ya kiungo wa kati tumeona kwamba hakuna wachezaji wazuri sana nyuma ya Yaya Toure na Fernandinho, huo ndio ukweli ambao unaonekana kudhihirika hususan katika kipindi hiki. Ndio, Demichelis ameshawahi kucheza katika nafasi ya kiungo wa kati wakati akiichezea Bayern Munich,
Lakini, katika misimu ya karibuni, Muargentina huyu ameweza kucheza nafasi ya beki. Katika mechi dhidi ya Chelsea, Demichelis alicheza katika nafasi ya kiungo wa kati.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe