Thursday, August 13, 2015


UKISIKIA la kuvunda halina ubani ndio huku. Ni baada ya straika wa zamani wa Yanga, Jerry Tegete, kulipiga teke fuko la fedha.
Ipo hivi; Kocha wa Coastal Union, Jackson Mayanja, alidhamiria kumsajili Tegete kutokana na kuvutiwa na kipaji chake na alikuwa tayari kufanya lolote ili straika huyo aichezee timu yake.
Lakini baada ya Tegete kumdengulia, ameamua kuachana naye. Tegete ametangaza kustaafu kucheza kwa mwaka mmoja.
“Tegete (Jerry) amenishangaza sana. Sijui tatizo ni nidhamu, kukata tamaa au kutojitambua. Sijaelewa kwanini hataki kucheza mpira wakati umri wake bado ni mdogo na ana kipaji kizuri,” Mayanja alisema.
“Mchezaji hawezi kustaafu kwa mwaka mmoja halafu akarejea uwanjani na kucheza katika kiwango kile kile. Mpira hauhitaji mapumziko ya aina hiyo. Kwanza mchezaji anapopumzika anaweza kuongezeka uzito haraka, lakini pia anakuwa na hatari ya kuendekeza mambo ya dunia.
“Sijui ni kivipi Tegete ataweza kurudi kiwanjani na awe vizuri. Nilimpa fursa na haitaki ingawa nilikuwa naamini ni mchezaji mzuri na angeweza kubadilika.”
Tegete ameliambia wazi Mwanaspoti kuwa hana mpango wa kucheza soka la ushindani kwa sasa na kwamba amepanga kuendelea na shughuli nyingine huku akidai kuwa amekataa ofa nyingi alizokuwa amepata kwa sababu hana mipango ya kucheza kwa sasa.
Tegete amekua akihusishwa na kujiunga na Mwadui lakini Coastal Union ilikuwa tayari kwa gharama yoyote kumnasa straika huyo wa zamani wa timu ya taifa ‘Taifa Stars’.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe