Thursday, June 26, 2014

KUTOKA LONDON: England ni kulaumiana tu


 
PAMOJA na kwamba Waingereza hawakutarajia timu yao ya taifa kutwaa Kombe la Dunia, lakini wamefadhaishwa na matokeo ya England katika mechi zake mbili za mwanzo.
Tangu Alhamisi hadi sasa mitaani jijini hapa, kwenye redio utitiri za FM za Uingereza gumzo ni timu ya Taifa ya England. Lawama nyingi zinaelekezwa kwa mabeki na kiungo licha ya kwamba hata ushambuliaji haujajijenga vyema.
Lawama pia zinatupwa kwa kocha, Roy Hodgson, kwa jinsi alivyokuwa akijitapa na kuwapa moyo washabiki kwamba wanakwenda kushindana hasa.
Baada ya kufungwa na Italia kwenye mechi ya kwanza, wakabamizwa tena na Uruguay 2-1, muuaji wao akiwa Luis Suarez.
Nakumbuka Alhamisi ile baada ya jina la Suarez, mpachika mabao wa Liverpool kutajwa kwenye orodha ya Uruguay, jamaa wengi niliokuwa nao waliguna kwa uchungu uliochanganyika na hasira.
Walihisi kwamba angewadhuru; hawakutarajia angecheza maana kwenye mechi ya Italia hakucheza na ni mwezi mmoja tu uliopita alikuwa akiburuzwa kwenye kiti cha magurudumu baada ya kuumia kwenye mechi ya Ligi Kuu England dhidi ya Newcastle.
Waingereza hapa wameudhika zaidi kwa sababu Suarez anacheza timu moja na nahodha wa timu ya taifa, Steven Gerrard na mshambuliaji mahiri, Daniel Sturridge.
Suarez ambaye mwaka 2010 aliizuia Ghana isifike robo fainali kwa kudaka mpira uliokuwa unatumbukia wavuni, anacheza pia na akina Raheem Sterling na beki Glen Johnson ambaye analaumiwa pia kwa kuwa uchochoro.
Maudhi ya Waingereza ni kwamba Suarez huyu huyu amewahi kudai kwamba Chama cha Soka England (FA) na vyombo vya habari vya hapa  havimpendi wala havimtendei haki na angetaka kwenda kucheza ligi ya nje ya hapa.
Lakini wangekuwa na kikosi imara hawangekuwa na sababu ya kusikitika kuona mchezaji fulani wa upinzani yupo wala sababu ya kuwapangia makocha wapinzani kikosi.
Nimesikia mashabiki wengi wakiwa na mawazo kwamba palikuwa na haja ya wachezaji wakongwe kujumuishwa kikosini.
Wanaona ilikuwa makosa kumwacha Ashley Cole hata kama ameshuka kiwango na pia wangemwita John Terry, nahodha wa zamani ambaye alisema angekuwa tayari kurudi kikosini kama angeitwa licha ya kutangaza kustaafu.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe