Wednesday, May 21, 2014

Wachezaji wa Timu ya Yanga wakiwa mazoezini.

KAMBI ya mmoja wa wagombea urais wa Simba, imeunda kamati ya usajili ambayo imeshafanya mazungumzo na wachezaji 35, lakini watachuja mpaka wabakie 12 na moja kati ya masharti iliyojiwekea ni kutomsajili mchezaji yeyote kutoka Yanga.
Jopo hilo ambalo linakutana mara kwa mara na kufanya shughuli zake kwa usiri mkubwa, linahusisha baadhi ya wajumbe waliopo kwenye kamati ya usajili ya sasa ya Simba ambao wanaamini kwamba mgombea huyo huenda akaingia madarakani.
Mmoja wa viongozi wa kamati hiyo ambaye hakupenda kutajwa jina lake gazetini kwa kuhofia kuwa lolote linaweza kutokea kwenye uchaguzi, alisema wameamua kufanya mchakato huo mapema ili wakiingia madarakani wasipate shida.
Tayari wameshazungumza na wachezaji 35 ambao wote wamekubali kujiunga na Simba lakini wenyewe watawachuja hadi kufikia 12 inayowahitaji kujumuisha na wale waliopo sasa kikosini.
Kamati hiyo imezungumza na kukubaliana kila kitu na wachezaji hao lakini mambo yakigeuka kila kitu kinawekwa pembeni. Katika vikao vyao vyote, kamati hiyo wamesisitizana kutosajili mchezaji yeyote kutoka Yanga kwani wanaamini wengi wanakuwa mamluki na huwa hawachezi kwa kujituma inapofikia timu inahitaji ushindi wa lazima.
“Lakini hatuwezi kuwasajili hadi uchaguzi upite, kama kambi yetu ikishinda mambo yataendelea kama yalivyopangwa lakini kinyume na hapo wataishia kuzungumza tu na viongozi wa Simba, hawataichezea Simba,” alisema mmoja wa viongozi wa kamati hiyo ambaye amewahi kusajili wachezaji wa Simba mara kadhaa.
Wachezaji wa Yanga waliomaliza mikataba yao ambao wanatajwa kuwa na mipango ya kujiunga na Simba ni kipa Ally Mustapha ‘Barthez’na beki wa kushoto David Luhende. Wote hao ni hitaji la Kocha Zdravko Logarusic ambaye katika ripoti yake ameusisitiza uongozi kusajili kipa atakayempa changamoto Ivo Mapunda na beki wa kushoto wa uhakika.
Banda naye aingia kundini
Katika mlolongo wa wachezaji hao wanaosajiliwa yumo beki wa Coastal Union, Abdi Banda, ambaye pia awali alikuwa akiwindwa na Yanga. Meneja wa mchezaji huyo Abdul Bosnia, alisema kuwa mazungumzo na mgombea mmoja wa nafasi ya juu kwenye uongozi wa Simba yanakwenda vizuri ingawa walimtaka amalizane na uongozi wa Coastal kwani mchezaji huyo bado ana mkataba wa mwaka mmoja.
“Kuna kiongozi wa Simba (anamtaja mgombea huyo) tunafanya naye mazungumzo kuhusu usajili, tumemwambia aonane na viongozi wa Coastal ambao ndiyo wamiliki wa mchezaji huyo, kila kitu kipo sawa hata ofa tuliyopewa ni nzuri ingawa tunajaribu kuiangalia zaidi.
“Banda ni mchezaji ambaye anaruhusiwa kuichezea timu yoyote, hata Yanga walikuwa wanamtaka ingawa kocha wao alimkataa ila mpaka leo (jana asubuhi) kuna kiongozi amenipigia kuuliza kama Simba wamemalizana na sisi,” alisema Bosnia.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe