Wednesday, May 21, 2014

Wachezaji wa timu ya Mbeya City.

KOCHA wa zamani wa Taifa Stars, Mshindo Msolla amesema timu sumbufu ya Mbeya City inavuna ilichokipanda baada ya kupata mwaliko wa kushiriki kwenye michuano mipya ya Cecafa Nile Basin yatakayoanza kutimua vumbi Alhamisi ya wiki hii.
Mbeya City ndiyo wawakilishi wa Tanzania Bara katika michuano hiyo ya Cecafa inayoshirikisha timu kutoka nchi zilizoko kwenye bonde la Mto Nile za Kenya, Sudan, Sudan Kusini, Tanzania, Uganda, Zanzibar, Misri, Ethiopia na Djibouti. Zanzibar itawakilishwa na timu ya Polisi Zanzibar.
Mbeya City ambayo imepangwa  na timu za AFC Leopards ya Kenya,  El Merreikh Al Fasher ya Sudan na  Elman ya Somalia katika kundi B, inashiriki mashindano ya Cecafa kwa mara ya kwanza baada ya kupanda daraja na kushiriki ligi kuu kwa mara ya kwanza msimu uliomalizika na kufanikiwa kumaliza katika nafasi ya tatu.
“Nawashauri tu wakapambane na wasiogope majina ya hizo timu kubwa kwani kama walivyoweza hapa nchini pia nje wataweza,” alisema Msolla aliyewahi kuifundisha Taifa Stars kabla ya ujio wa Mbrazil Marcio Maximo.
Kwa upande wake kocha msaidizi wa Mbeya City, Maka Mwalwisi alisema, “Hii kwetu ni changamoto mpya, tunakwenda kucheza na timu kubwa na zenye uzoefu wa kimataifa, natumai hiyo ni fursa kwetu sisi kujifunza zaidi.
“Mbali na kujifunza pia tutakwenda kupambana ili tuweze kuieperusha bendera ya nchi yetu vyema, kamwe hatutalala na kupoteza fursa hiyo,” aliongeza Mwalwisi.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe