Friday, May 2, 2014

 

Saad Kipanga. 

MSHAMBULIAJI wa Mbeya City, Saad Kipanga, amekiri kuwa Simba imemfuata na yeye amewapa masharti yake, kwanza wamkabidhi kitita cha Sh30 milioni akiweke kibindoni na mambo mengine wamalizane na uongozi wa klabu yake.
Kipanga ni yule mshambuliaji aliyekuwa anavalia jezi namba 27 mgongoni, mrefu na amejazia, wengi walikuwa wanamfahamu kutokana na staili yake ya kucheza soka ya kuvizia, huwa haeleweki ni nafasi gani ya ushambuliaji anayocheza uwanjani, kila kona anakuwepo.
Anasifa nyingine ya nguvu za miguu, mabao yake mengi ameyafunga nje ya 18 pamoja na akili ya mpira.
Akizungumza na Mwanaspoti, Kipanga alisema: “Mimi ni mchezaji wa Mbeya City na bado nina mkataba nao, ni kweli Simba wamenifuata na tuko kwenye mazungumzo ambayo kama mambo yataenda vizuri, nitamalizana nao.
“Lakini nimewapa masharti ambayo kwa upande wangu nahitaji shilingi milioni 30 na mambo mengine yanayobakia, wamalizane na klabu yangu ya Mbeya City kwa sababu bado nina mkataba nao.”
Kipanga alisajiliwa na Mbeya City usajili wa dirisha dogo na kucheza mzunguko wa pili kwa mkataba wa mwaka mmoja akitokea Rhino ya Tabora. Kwa kipindi hicho kifupi, ameng’ara na Mbeya City ambayo imemaliza ligi ikiwa nafasi ya tatu kwenye msimamo nyuma ya Azam FC ambao ndiyo mabingwa na Yanga washindi wa pili.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe