Friday, May 2, 2014

 

AZAM na Simba kwa nyakati tofauti zimeanza operesheni za kuimarisha timu zao kwa kufanya usajili ambao huendahatima yake ukaiachia Yanga kilio kikubwa. Azam tayari imeshamng’oa Didier Kavumbagu na sasa inamalizana na Frank Domayo na Mbuyu Twite.
Lakini Simba imepania kuwarejesha beki Kelvin Yondani na kipa Ally Mustapha ‘Barthez’ ambao wote ni wazoefu. Lakini pia inamwania straika mmoja mzalendo wa Jangwani ambaye haijataka kuliweka wazi jina lake.
Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga, aliliambia Mwanaspoti jana Jumatano kwamba wanamtaka Barthez kwa udi na uvumba na atatua Msimbazi kwa mkataba wa miaka miwili kama mambo yakienda kama yalivyo sasa.
Barthez amemaliza mkataba wake na Yanga na hakuwa na wakati mzuri kwenye kikosi hicho mwishoni mwa msimu uliomalizika baada ya kupoteza namba yake.
Kamwaga alisema kuwa kocha wao, Zdravko Logarusic, ndiye aliyependekeza Barthez asajiliwe ili kuongeza nguvu kwenye kikosi chao msimu ujao baada ya kuvutiwa na kiwango chake.
“Kocha ametaka msimu ujao awe na kikosi kisichozidi wachezaji 25 na katika mapendekezo yake pia amemtaja Barthez. Tumeshaanza mazungumzo na Barthez na huenda tukampa mkataba wa miaka miwili,” alisema Kamwaga ambaye ameanzisha operesheni Bunju kwa ajili kujenga uwanja wa Simba kwenye kiwanja chao kilichoko Bunju.
Imeelezwa kuwa Barthez ameshawaweka wazi Yanga kwamba anarudi Simba ambako alishawahi kusoteshwa benchi kwa miaka mitatu na Juma Kaseja kabla ya kutimkia Yanga na kupanda chati na kuwa kipa tegemeo ndani ya klabu hiyo, alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kufungwa mabao matatu katika mechi ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Simba iliyomalizika kwa sare ya mabao 3-3.
Lakini wakati Kamwaga akisema hivyo, siku moja kabla ya kwenda kwao Croatia mapumzikoni, Logarusic aliiambia Mwanaspoti kuwa amependekeza wachezaji sita pekee ndio wasajiliwe kwenye kikosi chake. Alisema anataka mabeki wawili, viungo wawili na washambuliaji wawili na kwamba alidai hataki wachezaji wa Yanga na Azam kwa vile wana majina makubwa na ni tatizo.
“Sitaki wachezaji kutoka timu kubwa, kwanza wanataka hela nyingi, halafu kurundika wachezaji wenye majina kunafanya timu haifanyi vizuri, sitaki wachezaji ambao wanatembea uwanjani huku wameshika viuno, nataka wachezaji wasio na majina kutoka timu ndogo naamini watanisaidia, nataka mchezaji shupavu wa kikosi cha kwanza sio mchezaji mwenye jina halafu anaanzia benchi,” alisema Loga.
Kamwaga alipoulizwa kuhusiana na kauli hiyo ya Loga, alisema: “Loga ndiye aliyempendekeza Barthez, ripoti yake wala haijasema kama hataki wachezaji kutoka timu hizo, yeye kapendekeza nafasi ambazo tunatakiwa kuzifanyia kazi, hivyo suala la usajili tumeliacha kwenye kamati ya usajili.
“Loga mwenyewe hatma yake ipo mikononi mwa uongozi mpya utakaoingia, tayari uongozi wa sasa umeshampa hela kidogo (kishika uchumba) ili asiende timu nyingine, lakini uongozi mpya unaweza ukaingia na kocha wao wanayemtaka na asiwe Loga kama watafanya hivyo uongozi wa sasa utakuwa umepoteza hela nyingi, lakini mwisho wa yote uongozi utakaokuja ndio utaamua kila kitu,” alisisitiza.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe