Wednesday, May 7, 2014

Aliyemuiba Domayo Yanga yupo hoi

YANGA wameanza mipango ya kuziba nafasi ya aliyekuwa kiungo wao Frank Domayo aliyehamia Azam FC,lakini huku nyuma bosi aliyefanya zoezi la kimafia kumsainisha nyota huyo ameugua.
Usajili wa Domayo ulianzia jijini Dar es Salaam ambapo mjomba wa kiungo huyo alikutana na mabosi wa juu wa Azam na kukubaliana kila kitu na hatimaye kuchukua fedha za malipo za ndugu yake.
Baada ya hilo kukamilika ikaja kazi ya pili ya nani atamsainisha mkataba Domayo aliyekuwa katika kambi ya Taifa Stars iliyopo Tukuyu, Mbeya. Baada ya tathmini fupi kazi hiyo akapewa mtu anayeitwa Jemedari Said Kazumali ambaye pia ni meneja wa kikosi akiongozana na wenzake wanne wakatua Mbeya kwa ndege ya haraka.
Kama lilivyo jina lake Jemedari aliifanya kazi hiyo na kiungo huyo akawa mali ya Azam ingawa baadae siku hiyo ilizuka tafrani iliyosababisha atiwe kizuizini na Askari wa Jeshi la Polisi ingawa hawakupelekwa kituoni.
Alipoachiwa na kurudi jijini Dar es Salaam baada ya siku mbili akaanza kuugua ghafla ambapo alilazimika kukimbizwa hospitali usiku ambapo alipumzishwa kutokana na hali yake katika Zahanati ya Arafa iliyopo Gongo la Mboto.
“Nimepumzishwa tangu jana usiku baada ya hali yangu kuwa mbaya sana, kikubwa ni malaria na tumbo, nilipofika hapa hospitali madaktari hawakutaka kuniruhusu kurudi nyumbani kutokana na hali yangu,” alisema Jemedari siku ya Jumamosi akiliambia Mwanaspoti.
Kidogo juzi hali ikabadilika ambapo Jemedari alirudi nyumbani ingawa hali yake haijatengamaa. “Nimerudi nyumbani lakini bado afya yangu haijaimarika sawasawa, sitaki kuhusisha kuumwa kwangu na mambo mengine lakini nasisitiza nipo ngangari waambie wote,” alisema Jemedari baada ya kuhisi kuna mkono wa mtu katika kuumwa kwake.
Wakati hali ikiwa hivyo kwake, mmoja wa mabosi wa juu wa Azam ambaye naye alihusika katika usajili Domayo (jina tunalo) naye alikuwa hoi kitandani nyumbani kwake akiugua mafua makali ambayo inasemekana hayajawahi kumshika katika kipindi cha miaka miwili.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe