Tuesday, April 29, 2014

Rais Kikwete aombwa kufuta hati shamba la mwekezaji

                         

Rais  Jakaya Kikwete ameombwa kufuta hati miliki ya sehemu ya eneo la mwekezaji wa kampuni ya Susumua Holdings ambalo ameshindwa kuliendeleza ili kuligawa kwa wananchi ambao hawana ardhi kwa ajili ya kilimo na ufugaji.

Ombi hilo lilitolewa na wananchi wa kijiji cha Kwamsisi, wilayani Handeni, wakati wa mkutano wa kijiji hicho uliokuwa ukizungumzia mgogoro uliopo baina ya mwekezaji wa kigeni na wananchi hao.

Walisema wanamuomba Rais Kikwete kuingilia kati mgogoro huo kwa kuligawa eneo ambalo mwekezaji amelihodhi bila ya kuliendeleza huku wakazi wa kijiji hicho wakiwa hawana sehemu ya kuendesha shughuli zao za kilimo na ufugaji.

Walidai mwekezaji huyo kwa sasa analima eneo dogo kwa ajili ya mazao huku akiacha karibu robo tatu ya shamba bila ya kuliendeleza kwa  kipindi kirefu jambo linalowafanya kuona hawatendewi haki na kuitaka serikali kufuta hati miliki ya  sehemu iliyobaki.

"Tunataka  ardhi hiyo igawiwe upya kwa wananchi kwani mwekezaji amekuwa akitukandamiza sisi wananchi kwa kujua tupo kijijini hapa akidhani hatuna uwezo wa akili kitu ambacho  hatutakubali  "alisema Makame Mwinyiheri.

Nae Afisa Mtendaji kata wa kijiji cha Kwedikwazu, Idrisa Nassor alisema mwekezaji huyo kila mara amekuwa akijiongezea eneo kwani awali alikuwa anamiliki ekari 6,174 na sasa amefikisha ekari 7,295.

“Tuna kaya zaidi ya 200 zinaishi ndani ya eneo lake ambazo zinakosa huduma muhimu hivyo tunaomba shamba lipunguzwe kwa ajili ya maslahi ya wananchi kuliko kutoa kwa wawekezaji wanao tuumiza ambao wanatusababishia kukosa huduma muhimu za kijamii" alisema Nassor.

Akizungungumzia malalamiko hayo ya wananchi, mwekezaji wa shamba hilo, Rony Nightngali alisema eneo hilo alimilikishwa kihalali na serikali kwa ajili ya kuendesha kilimo cha matunda na mbogamboga, lakini uwelewa mdogo wa masuala ya haki za umiliki wa ardhi kwa wanakijiji hao ndiyo unapelekea migogoro ya mara kwa mara .

Alisema kampuni yake imeamua kuwekeza karibu na maeneo ya kijiji hicho ili kutoa fursa za ajira kwa wananchi pamoja na kukuza pato la uchumi wao kutoka na kushiriki katika ulimaji wa mazao.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe