Monday, April 21, 2014

 

Rais Jakaya Kikwete  akiwa katika mahojiano maalumu na Mtangazaji Daniel Kalinaki wa Kituo cha Televisheni cha Nation (NTV) kinachomilikiwa na Nation Media Group, Ikulu jijini Dar es Salaam. Picha na Ikulu  

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete ameendelea kusisitiza kuwa Tume ya Jaji Joseph Warioba haina ushahidi kwamba Watanzania wengi wanataka muundo wa Muungano wa serikali tatu.
Kauli hiyo aliitoa wiki hii jijini Dar es Salaam kwenye mahojiano maalumu na Kituo cha Televisheni cha NTV kilichopo chini ya Nation Media Group (NMG).
Baadhi ya vyombo vingine vya habari vilivyo chini ya NMG ni gazeti hili la Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti kwa upande wa Tanzania, Daily Monitor kwa upande wa Uganda na Daily Nation kwa upande wa Kenya.
Rais Kikwete ambaye moja ya mambo atakayokumbukwa kwenye uongozi wake ni kuasisi mchakato wa Katiba, alizungumzia hoja ya serikali tatu akisema, hakuna ushahidi kwamba Watanzania wengi wanataka muundo wa Muungano wa serikali tatu.
“Hakuna ushahidi kwamba watu wengi katika nchi hii wanataka serikali tatu, hakuna ushahidi wa namna hiyo, hata tume yenyewe haikubaini hicho. Kinachofanywa na vyombo vya habari ni kuandika habari za wajumbe wa Bunge la Katiba wanaotaka serikali tatu, ndiyo kwenye masilahi yao, wanapaza sauti za wale wanaotaka serikali tatu, hao ndiyo sauti zao zinasikika. Lakini hawataki kupaza sauti za wale wanaotaka serikali mbili,” alifafanua.
Hii ni mara ya pili kwa Rais Kikwete kuikosoa ripoti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba. Mara ya kwanza aliikosoa wakati akizindua Bunge la Katiba Machi 21 mjini Dodoma.
Rais Kikwete ambaye amewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwa kipindi cha miaka 10, katika mahojiano hayo alisema katika kuadhimisha miaka 50 ya Muungano, jambo muhimu na kubwa ni kuendelea kuwapo kwa Muungano.
“Tunayo mifano ya nchi zilizojaribu kuungana, lakini zilishindwa, Senegal-Gambia, Ghana-Guinea, Misri na Libya.
“Muungano umeendelea kuwepo kwa nusu ya karne ni mafanikio makubwa. Kumekuwepo na wakati mgumu na changamoto mbalimbali, lakini tumeweza kukabiliana nazo na umeendelea kuwa imara zaidi. Siyo kuendelea kuwepo tu pia umeendelea kuimarika na mchakato wa mabadiliko ya Katiba utaimarisha zaidi Muungano na tutakuwa na Muungano imara baada ya kupata Katiba Mpya,” alifafanua Rais Kikwete.
Akizungumza kwa kujiamini kutokana na uzoefu wake wa muda mrefu ndani ya CCM na Serikali, Rais Kikwete alisema Muungano ulikotoka ulikuwa imara na umeendelea kukua katika hali ya uimara wake.
“Kuna mambo ambayo tumefanya yamezidi kuimarisha Muungano na umeendelea kuwa na mafanikio makubwa.”
Alisema suala si kuendelea kwa muundo ulivyo sasa, suala la msingi ni kujadili namna ya kutengeneza muundo wa Muungano, kwamba upi ni bora.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe