Monday, April 21, 2014

Mtikila ‘apiga hela’ mkutano wa Ukawa

Dodoma. Kiongozi wa Chama cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila, juzi alitoa mpya ya aina yake katika Mkutano wa Umoja wa Katiba ya Watanzania (Ukawa) pale alipopigia debe kitabu chake ambacho kilinunuliwa kwa idadi kubwa na wajumbe wenzake.
Kundi la Ukawa lilikuwa na mkutano wake wa kuweka mikakati kwenye Hoteli ya African Dreamer ikiwa ni siku moja baada ya kutoka nje ya Ukumbi wa Bunge Maalumu la Katiba linaloendelea mjini Dodoma.
Katika mkutano huo, Mchungaji Mtikila alikuwa mtu wa tano kuzungumza na sehemu kubwa ya hotuba yake ilikuwa ikiwalalamikia wajumbe wa CCM kuwa hawana nia ya kutengeneza Katiba na kazi yao ni kuwazomea na kushangilia hata anayeongea pumba.
Mtikila alisema kuwa wao kama Ukawa wanaona kwa hali iliyopo hakuna Katiba inayoweza kupatikana. “Kwa mazingira haya, hakuna Katiba itakayopatikana na kukubalika duniani, haipo,” alisema Mtikila.
Kabla ya kuhitimisha, Mtikila alitumia nafasi hiyo kutangaza kuwa ana kitabu kilichokuwa kikizungumzia hoja yake iliyokataliwa na Mwenyekiti wa Bunge ya kwanini mchakato wa Katiba usivunjwe.
“Halafu ndugu mwenyekiti, mimi nina kakitabu kangu, kadogo tu tumefanya kazi juzi na jana kukiandaa. Tulioshirikiana nao sasa wanataka kuja Dodoma kwa mguu, sasa kakitabu haka kako hapa, mnichangie. Nimechelewa nilikuwa kwa wale wachapaji,” alisema na kuongeza:
“Ni mambo ambayo Mheshimiwa Sitta aliwaambia waandishi wa habari nimenyimwa nafasi ya kutoa hoja binafsi kwa sababu nimegawa uchochezi kwa hiyo uko humo na ulipofika kwa wananchi, unafanya kazi takatifu kabisa...Hivi sasa niko kwenye kompyuta natengeneza kitu kizuri zaidi,” alisema Mtikila.
Baada ya kauli hiyo, wajumbe walianza kumiminika alipokuwa amekaa na kununua kama njugu vitabu hiyo vyenye kurasa 40.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe