Wednesday, March 12, 2014

       Al Ahly wambakiza Cannavaro Cairo

      Nadir Haroub ‘Cannavaro’ 

AL AHLY haijaamini kwamba imewang’oa Yanga kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika. Lakini baada ya kutimiza azma hiyo, itafanya usajili wa wachezaji wawili wapya muhimu.
Nyota hao itakaowanunua ni kiungo na beki safu ambazo zina utata mkubwa kwenye kikosi chao.
Jopo la usajili la Ahly limemtaja, beki kisiki wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kama mlengwa wao namba moja na wamemfanyia utafiti wa kina kwenye mechi zote mbili walizocheza na Yanga na watawasilisha maombi yao rasmi Jangwani kwavile wamevutiwa na uwezo wa mchezaji huyo kwenye kuzuia, kufunga na kuhamasisha.
Jana Jumatatu walikuwa na kikao kirefu na baada ya mazoezi ya jioni walitarajia kufikia muafaka na kuwasilisha maombi Yanga kabla ya haijakwea pipa usiku wa leo Jumanne na kuwasili Dar es Salaam kesho Jumatano alfajiri.
Mmoja wa viongozi wa Ahly aliyejitambulisha kwa jina la Mohammed Saed alisema tangu awali lengo lao ilikuwa ni kusajili beki na kiungo kama wangefanikiwa kuiondosha Yanga, lakini baada ya kukamilisha azma hiyo wanarudi mezani kuandaa utaratibu wa kuishawishi Yanga iwape mchezaji huyo aliyewafunga bao pekee la jijini Dar es Salaam.
Mohammed alisema wamepokea mapendekezo kutoka katika benchi lao la ufundi ambalo limemtaja moja kwa moja beki huyo huku wakimfikiria kiungo mmoja wa Yanga ambaye hakumtaja kwa madai kuwa wanasubiri ripoti nyingine ya benchi la ufundi kuhusiana na nafasi hiyo na ufanisi wa viungo wa Yanga kwenye mechi ya marudiano.
“Kuna nafasi ambazo tunatakiwa kuzifanyia maboresho yule beki wa Yanga anayevaa jezi namba 23 (Cannavaro) tunamhitaji lakini pia kuna kiungo mmoja ambaye tunasubiri tathmini ya kocha kwenye mechi ya marudiano tufanye uamuzi,”alisema Mohammed ambaye amekuwa mstari wa mbele kwenye mechi zote mbili za Dar es Salaam na Alexabdria.
Katika mazoezi ya mwisho ya Yanga kwenye Uwanja wa Max mjini Alexandria, mmoja wa wapiga picha wa televisheni ya timu hiyo alipewa kazi maalum ya kuchukua picha za Cannavaro tu wakati akijifua ambapo alikuwa akimfuatilia kwa karibu zaidi kuliko mchezaji yeyote.
Kocha msaidizi wa Ahly, Ahmed Ayoub alizungumza na Mwanaspoti jana Jumatatu na kukiri kumtaka beki huyo lakini akasisitiza kuwa uongozi wa juu ndio wenye mamlaka ya kutoa tamko kwavile wao kazi yao ni kupendekeza.
Yanga yazindua jezi
Katika mechi mbili dhidi ya Ahly, Yanga ilitumia jezi mpya za aina mbili ambazo ilithibitisha kwamba zimenunuliwa Uingereza.  Jijini Dar es Salaam ilitumia jezi mpya zilizokuwa na mistari ya njano na kijani ambazo hawakuwahi kuzitumia miaka ya karibuni.
Katika mchezo wa marudiano juzi Jumapili uliopigwa mjini Alexandria, Misri walitambulisha uzi mwingine mpya ambao hauna tofauti kubwa na jezi za timu ya taifa ya Brazil

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe