Wednesday, February 26, 2014

    Mafuriko ya Yanga yaisomba Simba Dar

   

MAFURIKO ya ushindi wa kishindo wa Yanga wa mabao 7-0 dhidi ya Ruvu Shooting juzi Jumamosi, jana Jumapili yaliizoa Simba kwenye Uwanja wa Taifa baada ya Mnyama kukubali kipigo cha mabao 3-2 mbele ya JKT Ruvu kwenye uwanja huo huo.
Simba waliingia uwanjani wakiwa na malengo mawili. Kwanza kujibu mapigo kwa Yanga kwa kuichapa kipigo cha maana JKT Ruvu ili kujikita kwenye nafasi ya tatu, lakini pili, kuisulubu timu hiyo ya jeshi ambayo katika mchezo uliopita ilipigwa mabao 6-0 na Prisons mjini Mbeya.
Wachezaji waliuchukulia mchezo huo laini lakini JKT walipoanza kushinda Simba wakapoteana na kumuacha Kocha mpya wa JKT Ruvu, Fred Minziro akicheka na kuonyesha mbwembwe za kila aina kwenye benchi lake.
Ukuta Simba
Ukuta wa Simba pamoja na makipa wao wameendelea kuigharimu timu hiyo baada ya kuruhusu mabao sita katika mechi nne mfululizo ambazo wameambulia pointi mbili huku Azam iliyokuwa kwenye uwanja wake wa Azam Complex, ikikubali sare ya mabao 2-2 mbele ya Prisons.
Matokeo ya jana yameibakisha Azam kwenye nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 37 na Yanga pointi 38 kileleni na Simba itaendelea kushika nafasi ya nne ikiwa na pointi 32 na Mbeya City nafasi ya tatu kwa pointi 35.
Katika mechi ya jana, ukuta wa Simba ulijengwa na mabeki Wiliam Lucian ‘Gallas’, Joseph Owino, Donald Mosoti na Henry Joseph ambaye alizidiwa kushoto na kusababisha JKT Ruvu kupata mabao yote kupitia upande wake.
Mabeki hao na makipa, Ivo Mapunda na Yaw Berko wameigharimu Simba tangu mechi yao ya Mtibwa Sugar ambayo walitoka sare ya bao 1-1, Mgambo Shooting walifungwa bao 1-0 na kutoka sare ya bao 1-1 na Mbeya City.
JKT walianza kuiandama Simba dakika ya sita kupitia kwa Idd Mbaga aliyekosa bao la wazi akiwa na Berko akishindwa kuunganisha pasi safi ya Amos Mgisa aliyemtoka Henry Joseph ambapo shuti la Mbaga lilidakwa na Berko huku mwamuzi David Paul akimpa kadi ya njano Damas Makwaya.
Wanajeshi wachachamaa
Wanajeshi hao walianza kuinyanyasa Simba kwa kuifunga bao la kwanza dakika 13 kupitia kwa Hussein Bunu aliyepokea pasi safi ya Mbaga, ingawa timu zote zilikuwa zikishambaliana kijanja na Amissi Tambwe akidhibitiwa na mabeki wa JKT.
Kocha wa Simba Zdravko Logarusic, aliamua kufanya mabadiliko dakika 22 kwa kumtoa Said Ndemla ambaye nafasi yake ilichukuliwa na Ally Badru. Dakika 29, Amri Kiemba alikosa mabao baada ya kupaisha mipira aliyotengewa na Haroun Chanongo huku mwamuzi akitoa kadi nyingine ya njano kwa Bunu wa JKT Ruvu ikiwa ni dakika ya 32 kwa kosa la kupiga mpira nje bila kujali filimbi.
                        
                            

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe