Friday, June 6, 2014


 

Tangu kutoka bungeni kwa Kundi la Wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananachi (Ukawa) kwenye Bunge la Katiba kwa madai ya kuchoshwa kwao na matusi, kejeli na ubaguzi, kumeibuka mijadala mikali, huku mawaziri na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa chama tawala CCM, wakivunja ukimya na kuamua kupambana na umoja huo kwa hoja kwenye hadhara.
Ni wazi sasa hatua hii inaonyesha bado kuna mivutano kutokana na kila upande kubeba na kutetea hoja zake na kutupiana lawama za kuukwamisha Mchakato wa Katiba Mpya.
Wakati Ukawa wakidai wabunge wa CCM ndiyo chanzo cha kuvuruga na kukwamisha mchakato huo, CCM wanaubebesha msalaba wa lawama Ukawa na kusema ni wakimbizi wa hoja walioshindwa kujenga ushawishi na kuamua kuweka mpira kwapani baada ya hoja zao kukosa mashiko.
Madai ya Ukawa wanaeleza kuwa CCM imeacha kujadili Rasimu ya Jaji Joseph Warioba iliyowasilishwa bungeni na kuonekana wakiwa na rasimu yao kibindoni, wakitaka matakwa yao ya kisera na kiitikadi yapitishwe na Bunge la Katiba kinyume na taratibu.
Ukawa wanakazia msimamo wao na kusema kwamba Muundo wa Muungano wa serikali mbili si pendekezo la Tume ya Jaji Warioba iliyowasilishwa katika Bunge hilo maalumu la Katiba.
Hata hivyo, madai mengine ya CCM yanaeleza kuwa kundi la Ukawa halina nia njema, limeshindwa kujenga ushawishi na kuonyesha uhalisia wa faida za muundo wa serikali tatu ikiwa ni pamoja na rasimu ya Warioba takwimu zake kujikanganya na kukosa uchambuzi yakinifu.
Wadadisi wa masuala ya kisiasa visiwani hapa wanaeleza kuwa kukwama kwa Mchakato wa Katiba, kunaweza kuendelea kuiweka Zanzibar katika mzingira magumu ya kiuchumi na kujikuta madai au kilio chao cha muda mrefu kikakosa mnyamazishaji wa kuwafuta machozi.
Pia wako wanaosema kuwa ni lazima Zanzibar ipate hadhi yake kamili ili kuwa na polisi wake, uraia, uhamiaji, hati za kusafiria, elimu ya juu, sarafu na benki kuu yake ili kujitegemea na kujiendeleza yenyewe.
Hali hiyo pia inapingwa na baadhi ya watu wanaosema hakuna mahali popote duniani ambapo nchi mbili zimeungana zikaendelea kuwa na mamlaka kamili na kuyataja madai hayo yana dhamira ya kuvunja Muungano na kuusambaratisha.
Mifano yao katika kuungana na kubaki na mamlaka moja kamili wanayafananisha mataifa ya Uingereza, Marekani, Ujerumani na India.
Kundi la wabunge wa Ukawa tayari limefanya mikutano miwili mikubwa ya hadhara katika Kisiwa cha Unguja na Pemba huku CCM ikifanya mikutano mitatu katika visiwa hivyo kwa nyakati tofauti wakihimiza msimamo wao kuwa ni sahihi.
CCM imeamua kuwapandisha majukwani mawaziri watano ili kuwajibu Ukawa wakiongozwa na Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, huku CUF kwa kutumia mwamvuli wa Ukawa, wamewapandisha viongozi wakuu wa vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF, NLD , DP na NRA ili kuweka msimamo wakiongozwa na Makamu wa Kwanza wa Zanzibar Rais Maalim Seif Sharif Hamad.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe