Thursday, June 12, 2014


Ndugu wa damu wakutana kwenye fainali mbili za Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza

JUNI 21 kwenye fainali za Kombe la Dunia za mwaka huu nchini Brazil kutashuhudiwa mechi itakayohusisha ndugu wawili wa damu wakiingia uwanjani kupambana. Hii ni wakati Ujerumani itakapomenyana na Ghana kwenye mechi za hatua ya makundi ya michuano hiyo.
Ndugu hao wa damu ni Jerome Boateng atakayekuwa upande wa Ujerumani anashindana na kaka yake Kevin-Prince Boateng atakayekuwa na kikosi cha Ghana kwenye mechi ya Kundi G.
Wakutana mara ya pili
Kwenye Kombe la Dunia, Jerome na Kevin-Prince wataendelea kuwa ndugu wa kwanza wa damu kucheza wakiwa timu pinzani. Wakati mwaka huu kwenye fainali hizo za Brazil wakiwa wamepangwa Kundi G sambamba na timu nyingine za Marekani na Ureno, mara ya kwanza ndugu hao kukwaana ilikuwa kwenye fainali za Kombe la Dunia 2010 zilizofanyika Afrika Kusini.
Mwaka huo, Ghana na Ujerumani zilipangwa pamoja Kundi D na timu za Serbia na Australia na kwenye mechi yao, Jerome alitoka kifua mbele kwa ushindi wa bao 1-0, shukrani kwa bao safi la kiungo Mesut Ozil dakika ya 60, ambaye pia alitajwa kuwa Mchezaji Bora wa Mechi.
Wote wanacheza Bundesliga
Kuhusu ndugu hao kuwa wapinzani kwenye mechi si kitu cha ajabu sana baada ya wote kucheza kwenye ligi ya Bundesliga ambapo timu zao zimekuwa zikichuana mara kwa mara.
Kevin-Prince anacheza kwenye klabu ya FC Schalke 04, wakati mdogo wake ni beki wa kutegemewa wa Bayern Munich, ambao msimu uliopita walinyakua mataji mawili, ubingwa wa Bundesliga na Kombe la Ujerumani.
Familia moja kwenye Kombe la Dunia
Fainali za Kombe la Dunia kushuhudia ndugu wawili wakicheza si kitu cha ajabu. Kwenye fainali za mwaka huu nchini Brazil, Ivory Coast itakuwa na ndugu kwenye kikosi chake, Kolo Toure na mdogo wake Yaya Toure.
 Kitu kama hicho kiliwahi pia kutokea miaka ya nyuma wakati Argentina ilipokuwa na ndugu Mario na Juan Evaristo, sawa na Mexico ilikuwa na ndugu Manuel na Felipe Rosas na Rafael na Francisco Gutierrez kwenye fainali za Kombe la Dunia mwaka 1930.
Baada ya miaka mingi ikaja zamu ya Fritz na Ottmar Walter, ambao waliisaidia Ujerumani kuibuka mabingwa nchini Uswisi 1954, kisha wakaja Bobby na Jack Charlton wa England kwenye Kombe la Dunia 1966 na Robert na Niko Kovac wa Croatia kwenye Kombe la Dunia 2002 nchini Japan na Korea Kusini. Lakini, hawa wote walikuwa wakicheza timu moja.
  

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe