Friday, June 6, 2014

Wachezaji wa timu ya Mbeya City

Dar es Salaam. Wakati Mbeya City wakisaini mkataba wa udhamini wa miaka miwili wenye thamani ya Sh360 milioni na kampuni ya Bin Slum Tyre Co. Ltd, wanachama wa Simba wametishia kumshtaki Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi kwa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), kwa madai ya kutaka kumpendelea mgombea urais wa klabu hiyo, Michael Wambura.
Mapema jana, Mbeya City ilisaini mkataba mnono wa Sh360 milioni wa kuifanya klabu hiyo kuingiza zaidi ya Sh500 milioni kwa msimu kutokana na udhamini pekee. Wanapata Sh100 milioni kutoka Azam Media kutokana na haki za televisheni, huku karibu Sh70 milioni zikitoka kwa wadhamini wakuu wa Ligi Kuu, Vodacom Tanzania.
Akizungumza wakati wa utiaji saini wa mkataba huo, mkurugenzi wa Bin Slum Tyre, Mohamed Bin Slum alisema wameidhamini timu ya Mbeya City baada ya kuona ina uongozi makini na ni timu yenye mafanikio makubwa.
“Uongozi umejipanga vizuri katika kuendesha timu yao kupata mwitikio mkubwa kutoka kwa wananchi wa Jiji la Mbeya na mikoa ya jirani,” alisema Bin Slum.
Naye katibu wa Mbeya City, Emmanuel Kimbe alisema imekuwa ni faraja kwa timu kwani itaweza kujiendesha na kufanya vizuri msimu ujao wa Ligi Kuu.
Kimbe alisema Mbeya City ina wajibu wa kuuthamini mchango huo uliotolewa na mdhamini kwa kuhakikisha inafanya vizuri zaidi msimu ujao. Kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya, Dk Samweli Lazaro alisema malengo ya timu yao ya kubadili mtazamo wa Simba na Yanga katika soka la Tanzania yametimia baada ya timu hiyo kupata mdhamini.
Wakati hayo yakitokea Mbeya, hali imekuwa tofauti kwa vigogo wa soka nchini, Simba baada ya wanachama watano wakiongozwa na Masoud Hassan (kadi namba 0500), Saleh Shahame (5596), Frank Pastori (02188), Rajabu Mtibu (01146) na Ally Mkumba (02519) kutishia kwenda Fifa kumshtaki Rais wa TFF, Malinzi, wakidai ameshatoa maelekezo kwa Kamati ya Rufaa za Uchaguzi ya shirikisho hilo inayotarajia kukutana Jumatatu ijayo na kusikiliza shauri la Wambura kupinga kuenguliwa kwenye uchaguzi wa Simba.
Akijibu madai hayo, Malinzi alisema msimamo wake wa kuitetea na kuilinda katiba na kanuni za TFF na wanachama wake uko palepale.
Malinzi alisema: “Sitegemei kumbeba mtu, ile kamati ni huru, itafanya kazi yake kwa uhuru kwa mujibu wa kanuni na katiba na si nje ya hapo.
“Wanaosema nina mpango wa kumbeba Wambura acha waseme. Ni demokrasia na hata kama wameenda Fifa pia ni sawa. Demokrasia inawaruhusu, siwezi kuwazuia.”
Wambura, ambaye amekumbana na panga kila anapojaribu kugombea uongozi wa soka kuanzia ngazi ya klabu hadi taifa, alienguliwa Simba kwa kuvunja katiba.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe