Wednesday, May 28, 2014


Mbeya City

TIMU sumbufu ya Mbeya City leo itaingia vitani kupambana na AFC Leopards kutoka nchini Kenya kutupa karata yake ya pili kuwania kufuzu robo fainali ya michuano ya Cecafa Nile Basin inayoendelea nchini Sudan.
Katika mchezo wa kwanza, Mbeya City iliichakaza Academie Tchite ya Burundi kwa mabao 3-2. Mabao ya Mbeya City yakiwekwa kiamiani na Paul Nonga, Mwagane Yeya na Temi Felix aliyesajiliwa kutoka Kagera Sugar wiki iliyopita.
Endapo Mbeya City inayoshiriki michuano ya kimataifa nje ya mipaka ya Tanzania kwa mara ya kwanza, itaibuka na ushindi kwenye mchezo huo wa leo itajipatia tiketi ya kucheza robo fainali ya michuano hiyo.
Mbeya City itacheza mechi yake ya mwisho ya hatua ya makundi dhidi ya Enticelles ya Rwanda kesho kutwa Jumatano.
Kipa wa Simba, Ivo Mapunda amesema endapo timu hiyo inahitaji kuibuka na ushindi dhidi ya Chui hao wa Kenya wanatakiwa kujiamini na kucheza kwa kupambana bila kuogopa jina la wapinzani wao.
Ivo ambaye ana uzoefu na timu za Kenya baada ya kucheza Ligi Kuu ya nchi hiyo kwa miaka miwili alisema, “Leopards ni timu ya kawaida, hawazidi sana uwezo Mbeya City bali wana uzoefu zaidi wa michuano ya kimataifa, naamini kama Mbeya City watatulia na kucheza kwa kujiamini wanaweza kuibuka na ushindi,” alisema Ivo.
Wakati Temi akianza kwa makeke katika timu yake mpya, Kocha Msaidizi wa Kagera Sugar, Mlage Kabange amesema mshambuliaji huyo ngongoti ana uwezo wa kuwapiku mastraika waliopo klabuni hapo na kupata nafasi ya kucheza kwenye kikosi cha kwanza.
Temi aliichezea Kagera kwa miaka 10, alisajiliwa na Mbeya City mwishoni mwa wiki iliyopita hivyo kujipa changamoto mpya ya kuchuana na mastraika wengine Saad Kipanga, Mwagane Yeya na Richard Michael ili kupata nafasi kucheza.
Kabange alikiri kuwa kuondoka kwa Temi kwenye kikosi cha timu hiyo ni pigo kutokana na uzoefu aliokuwa nao klabuni hapo na uwezo aliokuwa akiuonyesha msimu hadi msimu hususani katika upachikaji wa mabao.
Temi aliifungia Kagera Sugar mabao 10 msimu uliopita licha ya kusumbuliwa na majeraha ya hapa na pale.
“Mbeya City na Kagera zina tofauti kidogo halafu pale Mbeya kuna wachezaji waliotoka na timu mbali na kucheza kwa muda mrefu kwa pamoja, hiyo ni changamoto kwa Temi ila itabidi aweke bidii ya kuzoea mazingira na mfumo.
“Ni imani yangu kuwa uzoefu alionao kwenye ligi kwa takribani miaka 10 sasa utambeba, nadhani hiyo pia ndio sababu kubwa iliyosababisha Mbeya City kumsajili, ni mchezaji mzuri na anafahamu kipi cha kufanya kwa wakati gani,” alisema Kabange.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe