Thursday, May 8, 2014

Migomo Mbeya inaongeza umaskini

Kwa kipindi cha miezi minne hadi Aprili mwaka huu, wafanyabiashara wa maduka na daladala jijini Mbeya wamefunga shughuli zao kwa dharura karibu mara tano.
Mbali ya kufunga biashara, watu mbalimbali wakiwamo wageni kutoka wilaya na mikoa mingine wameathirika na matukio hayo kutokana na kukosa huduma muhimu zikiwamo za usafiri na hata bidhaa muhimu kwa maisha.
Sababu za kufunga ni kuwapo kwa tishio la vurugu au kwa madai ya kufanya mikutano ya dharura kunakoandamana na migomo baridi.
Kwa mara ya kwanza Februari walifunga maduka baada ya kufumuka vijana waliokuwa wakizunguka mitaani wakidai wanapinga mpango wa Serikali kuwataka wafanyabiashara watumie mashine za kutoa risiti zenye mfumo wa kielektroniki.
Wafanyabiashara walifunga maduka yao kwa siku mbili na mara ya pili ilitokea Machi kwa madai hayohayo na polisi walilazimika kupiga mabomu kuwatawanya vijana walikuwa wakitaka kufunga barabara.
Kana kwamba haitoshi, mwanzoni mwa Aprili wafanyabiashara walilazimika kufunga maduka yao baada ya vijana wa bodaboda kuanzisha kizaazaa kwa madai ya kutaka kupambana na polisi waliokuwa wakimwokoa mtu aliyedaiwa kushiriki kumuua mwendesha pikipiki maeneo ya Airport jijini hapa.
Nao madereva wa daladala mwishoni mwa Aprili walikunjua makucha baada ya kusitisha kutoa huduma kwa madai wako kwenye mkutano wa kujadili sababu za uongozi wa jiji kuwalazimisha daladala zipitie kwenye Soko la Soweto na eneo la Block T.
Kwa jumla wakazi wa aina mbalimbali katika Jiji la Mbeya wanaishi maisha yasiyotabirika. Migomo ama vurugu inawazidishia ukali wa maisha. Wanaofanya maisha yawe mabaya ni wale wanaoshiriki kuhamasisha wenzao wafunge biashara.
Kufunga biashara ama kuacha kubeba abiria kunakwamisha mzunguko wa fedha kwa watu mbalimbali. Kama mwenye daladala alitarajia kupata Sh30, 000 kwa siku husika, akigoma fedha hizo hazitampitia.
Kwa mfano tukio la mwishoni mwa Aprili daladala zinazofanya safari kati ya Igawilo, Uyole hadi mjini zilisitisha huduma kwa siku mbili watu wengi wakiwamo wake wa madereva walilalamika kukosa fedha.
Hali kadhalika wanafunzi, wafanyakazi walilazimika kushikilia fedha zao mfukoni ambazo walizipanga kwa nauli zao. Kana kwamba haitoshi watu wengi waliotaka kununua bidhaa madukani walishindwa kufanya hivyo kutokana na kukosekana usafiri.
Pia wenye maduka wakiyafunga watambue wazi kwamba wanakosa fedha ambayo hawakuitarajia na kamwe hawataipata tena fedha ile.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe