Wednesday, May 21, 2014


MANCHESTER, ENGLAND
MANCHESTER United sasa ikae mkao wa kusubiri mastaa wa maana msimu ujao. Arjen Robben, Thomas Muller, Mats Hummels, Luke Shaw na Toni Kroos watavaa uzi wa miamba hiyo ya Old Trafford baada ya jana Jumatatu kusimikwa rasmi kwa Mdachi Louis van Gaal kuwa kocha mkuu wa kikosi hicho.
Kabla ya kuchaguliwa kuwa kocha klabuni hapo, Van Gaal alimwambia bosi wa miamba hiyo makamu mwenyekiti, Ed Woodward orodha ya vitu anavyotaka vifanywe ikiwamo usajili wa mastaa hao makini, ambao anadai ni lazima wasajiliwe.
Wiki iliyopita, Woodward alisema pesa za kufanya usajili huo hazina tatizo, zipo tayari na nia ya kufanya hivyo ipo jambo kwamba wanatazamia kuingia hasara ya pauni 37 milioni kwa msimu ujao kutokana na kukosa Ligi ya Mabingwa Ulaya ikiwa ni mara ya kwanza tangu msimu wa 1995-1996 na pia inakosa soka la Ulaya kwa mara ya kwanza baada ya miaka 25.
Kwenye uteuzi huo, Van Gaal atasaidiwa na mkongwe wa klabu hiyo Ryan Giggs, ambaye awali alikuwa kocha wa muda baada ya kutimuliwa kwa David Moyes aliyedumu na miamba hiyo kwa miezi 10 pekee tangu alipomrithi Sir Alex Ferguson mwaka jana.
Makocha wengine waliokuwa wakihusishwa na kibarua hicho cha kuinoa Man United ni Carlo Ancelotti na Jurgen Klopp, lakini uteuzi wa Van Gaal unaweza kupokelewa kwa furaha na mashabiki wa timu hiyo hasa kutokana na matakwa yake kwamba klabu ni lazima isajili wachezaji makini wenye hadhi ya kucheza Man United.
Van Gaal ni mfuasi wa soka la kushambulia na hilo ndilo linalomfanya atake mastaa ambao wataifanya Man United icheze mpira wa maana msimu ujao na si kubahatisha. Mdachi huyo amesaini mkataba wa miaka mitatu na miamba hiyo na ataanza kibarua rasmi Old Trafford baada ya kukiongoza kikosi cha Uholanzi kwenye fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil zitakazoanza mwezi ujao.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe