Friday, May 2, 2014

AZAM KUFURU KUBWA, Yachukua injini ya Yanga, Jangwani wajibu mapigo

 

Frank Domayo akisaini mkataba wa miaka miwili wa kuichezea timu ya  Azam FC msimu ujao, msimu uliopita alikuwa akiichezea Yanga.

INJINI ndio roho ya gari aina yoyote ile, hakuna gari linaloweza kutembea wala kuwaka kama likitolewa injini. Azam FC imeng'oa injini ya kikosi cha Yanga.
Imemsainisha straika, Didier 'Mabao' Kavumbagu na Frank Domayo na sasa imetunisha misuli kwa nyota mwingine mmoja ambao kama wote waking'ooka tu,  Yanga kitanuka.
Jana Jumatano mapema tu Azam ilianza mazungumzo na kiungo ambaye ni kama injini ya Yanga, Frank Domayo na kiraka Mbuyu Twite na ilipofika saa 1:30 usiku, ilifanikiwa kuinasa saini ya Domayo. Domayo ambaye yupo kwenye kambi ya Taifa Stars iliyopigwa Tukuyu, Mbeya alizungumza na viongozi hao wa Azam mapema na kumalizana kabla ya kumfuata kwenye kambi ya timu ya taifa na kumsainisha  mkataba wa miaka miwili.
Domayo amemwaga wino kuichezea Azam FC kwa mkataba wa miaka miwili baada ya kumaliza mkataba wake wa miaka miwili katika klabu yake Yanga aliyojiunga nayo miaka miwili iliyopita akitokea JKT Ruvu ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Twite kwa upande wake alikuwa na mazungumzo na Azam na Yanga jana Jumatano mchana na jioni na alikiri kwamba Azam wamemuahidi mambo mazuri. Habari za uhakika ambazo Mwanaspoti imezipata ni kuwa Azam imepania kuwang'oa nyota hao, lakini Yanga na wenyewe wameweka mtego kwa kiungo makini wa Azam, Salum Aboubakary 'Sure Boy'. Hata hivyo, habari za kutoka ndani ya Azam zinabainisha kwamba Sure Boy ana mkataba wa miaka miwili hivyo itakuwa ngumu kwa Yanga kulipa kisasi kwa kumsajili kiungo huyo.
Akizungumza na Mwanaspoti, Meneja wa Azam, Jemedari Said,  alisema kwa mujibu wa ripoti ya Kocha Mkuu wa timu hiyo Mcamerooni, Joseph Omog, Azam inataka wachezaji sita kwa ajili ya kukiimarisha kikosi kiweze kucheza kiushindani Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani.
"Katika ripoti ya kocha tuliyoipokea, inaagiza kuwa tusajili kiungo wa kati mwenye kiwango kikubwa cha kucheza nafasi hiyo, mawinga wawili kushoto na kulia na kipa mwenye uzoefu wa kimataifa na hata beki wa pembeni hasa kulia.
"Yupo Manula (Aishi) mwenye uwezo mkubwa, lakini yeye hana uzoefu wa kucheza mechi za kimataifa, hivyo tunaendelea na usajili wetu wa kimya kimya kama tulivyofanya kwa Kavumbagu," alisema Jemedari ambaye aliwahi kuichezea Simba.
Kavumbagu aliiambia Mwanaspoti kuwa hatashangaa akisikia Twite amesaini Azam kwa vile Yanga bado hawaeleweki na amekuwa karibu na Twite anajua kila kinachoendelea.
Twite alipotafutwa kuzungumzia hilo, alisema: "Kiukweli kabisa, Azam nimepanga kukutana nao leo (jana Jumatano) jioni kwa ajili ya kusaini mkataba wa kuichezea timu hiyo.
"Yanga wameniita nimepanga kukutana nao kwa ajili ya mazungumzo ya kusaini mkataba mpya, majibu kamili nitayatoa mara baada ya kukutana nao wote."
Hata hivyo Twite na alipotafutwa baadaye jioni, akasema kwamba hawajafikia muafaka.

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe