Saturday, April 5, 2014

RAMSEY IS BACK: Yupo tayari kuivaa Everton 

 

LONDON, ENGLAND
WALAU mashabiki wa Arsenal na kocha wao, Arsene Wenger, wanaweza kupumua kama kiungo, Aaron Ramsey, atarudi uwanjani na kiwango kilekile alichokuwa nacho wakati wa raundi ya kwanza ya Ligi Kuu England.
Wenger ametangaza kwamba kiungo huyo wa kimataifa wa Wales,  anatarajiwa kurudi uwanjani kesho Jumapili katika pambano muhimu la kwania kuingia Top Four dhidi ya Everton litakalofanyika uwanjani  Goodson Park jijini Liverpool.
Ramsey hajaichezea Arsenal mechi yoyote tangu Desemba 26 mwaka jana wakati walipoibamiza West Ham mabao 3-1 na alitarajiwa kuwa nje kwa wiki sita kutokana na maumivu ya misuli ya paja, lakini muda huo ukaongezeka baada ya kujitonesha wakati akiwa katika harakati za kurudi uwanjani.
Nyota ya Ramsey msimu huu imeng’ara kwa kiasi kikubwa na katika raundi ya kwanza alikuwa amefunga mabao 13 ya Ligi Kuu England na tangu alipoumia Arsenal imeyumba kwa kiasi kikubwa katika eneo la ushambuliaji.
Beki wa pembeni wa Arsenal, Nacho Monreal, naye anaweza kucheza Goodison Park huku kiungo Abou Diaby ambaye yuko nje ya uwanja karibu mwaka mmoja sasa akikaribia kurudi baada ya maumivu makubwa ya goti.
“Aaron na Nacho Monreal wamerudi katika mazoezi, hizo ni habari nzuri. Nina matumaini watapatikana Jumapili. Diaby amerudi uwanjani kwa hiyo na hizo ni habari njema,” alisema Wenger.
Viungo Jack Wilshere na Mesut Ozil bado wako nje ya uwanja, lakini beki wa kati Laurent Koscielny anaweza kurudi wiki ijayo katika pambano la nusu fainali ya Kombe la FA dhidi ya Wigan. Hiyo ni baada ya kuanza kupata nafuu katika maumivu ya kiazi chake cha mguu.
Wenger amekiri kwamba itakuwa mapema kumrudisha Ozil katika pambano dhidi ya Wigan, lakini Ozil mwenyewe ameandika katika ukurasa wake wa Facebook kuwa amepania kurudi uwanjani akiwa katika kiwango  na kwa wakati mwafaka.

 

0 comments:

Post a Comment

Designed by Adamu Mwanakatwe